Lissu: Walipotelea wapi waasisi sita wa Muungano - Kitoloho
Headlines News :
Home » » Lissu: Walipotelea wapi waasisi sita wa Muungano

Lissu: Walipotelea wapi waasisi sita wa Muungano

Written By Msamaa on Thursday, May 15, 2014 | 12:51 AM

 


Dodoma. 



Serikali imetakiwa kutoa maelezo bungeni, kuhusu sababu za kuuawa kwa waasisi sita wa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar wanaodaiwa kuzikwa katika handaki moja Zanzibar.
Akiwasilisha maoni ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano), msemaji wake, Tundu Lissu aliitaka Serikali kueleza waasisi hao walifanya makosa gani.
Aliwataja waasisi hao kuwa ni Abdallah Kassim Hanga aliyekuwa Waziri Mkuu, Abdulaziz Twala aliyekuwa Waziri wa Fedha na Saleh Akida aliyekuwa Mjumbe wa Baraza la Mapinduzi na viongozi waandamizi wa Serikali ya Mapinduzi, Othman Shariff, Mdungi Ussi na Jaha Ubwa ambao alisema waliuawa na kuzikwa handaki moja eneo la Kama, Zanzibar.
Lissu alisema hayo huku akinukuu kitabu cha ‘Kwaheri Ukoloni, Kwaheri Uhuru’ kilichoandikwa na Harith Ghassany alichosema kilionyesha jinsi viongozi hao walivyouawa na kuzikwa katika kaburi moja.
“Sisi wa kizazi cha Muungano tunataka kujua ukweli juu ya makosa waliyoyafanya hawa waasisi wa Muungano hadi wakauawa na kuzikwa katika kaburi au handaki moja,” alisema Lissu huku wabunge wakiwa kimya kumsikiliza.
Mgawo wa Zanzibar
Lissu pia aliibua mambo mazito kuhusu mgawanyo wa fedha za misaada na mikopo ya kibajeti kati ya Serikali ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.
Alisema Muungano ni kielelezo cha unyonyaji na ukandamizaji ambao nchi kubwa imeifanyia nchi ndogo ya Zanzibar kwa miaka mingi.
Alikwenda mbali na kuitaka Serikali ya Mapinduzi Zanzibar au Wazanzibari kwa umoja wao, kufungua kesi Mahakama za kimataifa kudai fedha zote ambazo nchi yao imeibiwa kwa kivuli cha Muungano.
Mbunge huyo ambaye pia ni Mwanasheria Mkuu wa Chadema, alisema hadi Machi mwaka huu, Zanzibar ilikuwa imepata gawio la Sh27.1 bilioni badala ya Sh32.6 bilioni zilizoidhinishwa na Bunge, sawa na asilimia 83.
Hata hivyo, alisema hilo linaweza lisiwe tatizo, kwani kwa mwelekeo wa takwimu hizo, hadi kufikia mwisho wa mwaka huu wa fedha, gawio lililoidhinishwa linaweza kuwa limelipwa lote.
Haya hivyo, alisema tatizo kubwa na la msingi ni kwamba, gawio lililoidhinishwa na Bunge si halali kwa Zanzibar, kwa mujibu wa hotuba ya Waziri wa Fedha, Saada Mkuya ya Aprili 30, mwaka huu.
 
Lissu alimnukuu Mkuya akisema mapato halisi ya Serikali ya Muungano yanayotokana na misaada na mikopo nafuu ya nje kwa mwaka 2013/2014 yalikuwa Sh1.163 trilioni.
“Kama Zanzibar ingepatiwa asilimia 4.5 ya mapato hayo kama inavyotakiwa kwa mujibu wa sheria, kwa mwaka jana pekee, gawio halali la Zanzibar lingekuwa Sh52.335 bilioni,” alisema.
“Badala ya kupatiwa Sh52.335 bilioni ambazo ni fedha zake halali, Zanzibar iliidhinishiwa Sh32.62 bilioni au asilimia 52 ya fedha zake halali. Hii ni sawa na asilimia 2.8 ya fedha zote za misaada badala ya asilimia 4.5.”
Alisema kwa ushahidi huo wa nyaraka za Serikali, kwa mwaka jana pekee Zanzibar iliibiwa Sh25.145 bilioni sawa na asilimia 48 ya fedha zake halali za gawio la misaada na mikopo ya kibajeti.
Kutokana na hali hiyo, kambi hiyo imeitaka Serikali kueleza ni kwa nini fedha halali za Zanzibar kutokana na misaada na mikopo ya kibajeti hazijalipwa kwa mwaka jana wa fedha.
Pia kambi hiyo imeitaka Serikali kupeleka mbele ya Bunge, takwimu za fedha zote za misaada ilizopokea na mikopo ya kibajeti kwa kipindi cha miaka 10 iliyopita.
Katika takwimu hizo, kambi hiyo imeitaka Serikali kueleza katika fedha hizo, ni kiasi gani kililipwa kama kwa Zanzibar kama gawio lake katika kipindi hicho kwa fedha za misaada na mikopo ya bajeti.
Kuhusu misaada na mikopo isiyokuwa ya kibajeti, Lissu alisema: “Ukweli ni kwamba hali ni mbaya zaidi kuhusu fedha za misaada na mikopo isiyokuwa ya kibajeti. Hapa pia takwimu za Serikali hii ya CCM zinatisha na kusikitisha.”
Alitolea mfano kuwa Mwaka wa Fedha 2013/2014 fedha za nje kwa ajili ya miradi ya maendeleo zikijumuisha misaada na mikopo zilikuwa Sh2.692 trilioni.
“Fedha hizi zote zilitumika kwa ajili ya miradi ya maendeleo ya Tanganyika. Zanzibar haikupata kitu chochote,” alisema Lissu ambaye pia ni Mbunge wa Singida Mashariki.
Lissu alisema kutokana na Muungano, Zanzibar imenyang’anywa mamlaka ya kuomba mikopo au misaada kutoka nje bila kibali cha Wizara ya Fedha ya Muungano.
“Sisi tuliozaliwa ndani ya Muungano tunataka kujua unyonyaji na wizi huu wa fedha za Wazanzibari utakomeshwa lini?” alihoji Lissu.
 
Waziri afafanua
Wakati Lissu akisema hayo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano), Samia Suluhu Hassan alisema kati ya Julai Mosi, 2012 na Machi mwaka huu Zanzibar imepata gawio la Sh36.75 bilioni kutokana na Kodi ya Mishahara ya Wafanyakazi (Paye).
Waziri Hassan alisema hatua hiyo ni baada ya mawaziri wa pande mbili kukaa na kukubaliana kuwa SMZ inastahili kwa vile kodi ya mapato inayotokana na mishahara ya wafanyakazi ni suala linalohusu mapato ya Muungano.
Hata hivyo, alisema marekebisho ya Sheria ya Kodi ya Mapato kuhusu kodi ya mishahara yanahitajika ili kuweka utaratibu wa wazi zaidi.
Pia alisema kuanzia Julai, 2013 hadi Machi mwaka huu, SMZ imepokea kodi ya mshahara ya Sh15.75 bilioni na fedha za Mfuko wa Maendeleo ya Jimbo Sh1.24 bilioni.
Kuhusu gawio la mapato ya misaada ya kibajeti, Waziri Hassan alisema SMZ imepata Sh27.19 bilioni kati ya Sh32.63 bilioni zilizoidhinishwa na Bunge kwa Mwaka wa Fedha 2013/14.
Alisema Serikali pia iliichangia SMZ Sh600 milioni kwa ajili ya kufanikisha maadhimisho ya miaka 50 ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Waasisi na Picha
Lissu alisema kuna jambo linalofikirisha sana kuhusu picha za miaka 50 ya Muungano, kwa kuwa baadhi ya watu wanaoonekana katika picha hizo wamefutwa katika historia wanayofundishwa watoto shuleni.
Alitolea mfano picha ya Mwalimu Julius Nyerere na Sheikh Abeid Karume wakisaini hati za makubaliano ya Muungano wakiwapo viongozi waliokuwa wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.
“Kwa upande wa Tanganyika alikuwapo Oscar Kambona, Bhoke Munanka na Job Lusinde, wakati kwa Zanzibar wanaoonekana ni Abdallah Kassim Hanga, Abdulaziz Twala na Ali Mwinyigogo,” alisema.
Lissu alisema Ghassay katika kitabu chake ameonyesha jinsi waasisi hao walivyotoa mchango mkubwa katika kufanikisha Mapinduzi ya Zanzibar ya Januari 12, 1964.
“Baadaye viongozi hao walifanikisha Muungano wa Zanzibar na Tanganyika Aprili 26 ya mwaka huo,” alisema na kuongeza kuwa hilo lilithibitishwa pia na aliyewahi kuwa Rais wa Zanzibar, Aboud Jumbe.
Lissu alisema katika kitabu chake, Jumbe ameeleza kuwa Kambona, Munanka na Lusinde ndio waliompelekea Karume nakala za hati ya makubaliano na kusainiwa Aprili 22, 1964.
 Chanzo: Mwananchi (Na Daniel Mjema na Sharon Sauwa, Mwananchi; Posted  Jumanne,Mei13  2014  saa 24:0 AM)
Share this article :

0 comments:

Speak up your mind

Tell us what you're thinking... !

ZILIZOSOMWA SANA.

Followers

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Proudly powered by Blogger
Copyright © 2011. Kitoloho - All Rights Reserved
Template Design by Creating Website Published by Mas Template