Kardinali Pengo akoleza msako-Mauaji Padri Mushi. - Kitoloho
Headlines News :
Home » » Kardinali Pengo akoleza msako-Mauaji Padri Mushi.

Kardinali Pengo akoleza msako-Mauaji Padri Mushi.

Written By Msamaa on Friday, April 5, 2013 | 1:56 PM



Kardinali Pengo akoleza msako.


Toleo la 282

20 Feb 2013


Sheikh alonga nchi za nje zimetia mkono

Kanisa jingine lachomwa Zanzibar

KAULI ya Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, kwamba serikali imezembea kutekeleza wajibu wake, uzembe ambao moja ya matokeo yake ni kuuawa kwa risasi kwa Padri wa kanisa hilo, Evaristus Mushi, imezua mgongano wa kimjadala miongoni mwa maofisa waandamizi serikalini, Raia Mwema, limeelezwa.

Kwa mujibu wa vyanzo kadhaa vya habari, baadhi ya maofisa waandamizi wamelazimika kujadili kauli hiyo, sambamba na kupima athari au faida zake katika operesheni inayoendelea ya kuwasaka wahusika wa tukio hilo.

Hatua ya maofisa hao imetokea saa kadhaa baada ya Pengo kuzungumza na vyombo vya habari na Raia Mwema ikielezwa ya kwamba, mabishano yamejitokeza miongoni mwa maofisa hao.

“Imebainika kuna baadhi ya taarifa ambazo hazikuwa zinafikishwa katika eneo husika, wakubwa (maofisa waandamizi wa masuala ya usalama) wamelumbana. Wengine inadaiwa walikuwa wakifikishiwa taarifa za dalili mbaya lakini hawakuwa wepesi kuchukua hatua, ni kama vile wamelewa kuendelea kufanya kazi katika nchi iliyojaa amani kila siku,” kilieleza chanzo chetu cha habari.

Katika mazungumzo yake na waandishi wa habari kuhusu tukio la kuuawa kwa Padri Evaristus Mushi wa Parokia ya Mtakatifu Joseph ya Mjini Magharibi, Unguja, Zanzibar, Pengo alitoa maelezo yanayotilia shaka kwamba mauaji hayo yana mkono wa baadhi ya watu wanaojitambulisha kwa jina la Kundi la Kidini la Uamsho.

Kwenye mazungumzo hayo yaliyofanyika jijini Dar es Salaam, Pengo alisema; “Tunahitaji rehema (za Mwenyezi Mungu) ili tuendelee kuwapo. Tunahitaji utulivu na kuelezana ukweli. Na endapo mmoja wetu atazembea, ni jukumu kuambiana kwamba hapo umezembea na utalifikisha Taifa pabaya.”

Kwa mujibu wa maelezo hayo ya Pengo, wauaji hao walipanga na kutekeleza unyama wao huo kutokana na uzembe na udhaifu wa vyombo vya dola kwa kushindwa kusoma alama za nyakati, kwa kuwa tayari wauaji hao walikwishasambaza vipeperushi vilivyoashiria dhamira hiyo mapema.

“Watu wanasema kikundi cha Uamsho kule Zanzibar ni kikundi cha kidini, lakini kinatoa vipeperushi kama hiki (alikionyesha kwa waandishi) ambacho kimenifikia mkononi. Kwa hiyo, ni wazi kuwa hadi kinifikie mimi, Watanzania wengi watakuwa wamefikiwa na kipeperushi hicho…inathibitisha kwamba vipeperushi hivi ni vya Uamsho, lakini si kazi yangu kuhakikisha (kuthibitisha) tamko la Uamsho ni la Uislamu, siamini kwamba vyombo vya usalama vya taifa letu vinaweza kusema havina habari,” alieleza Pengo.

Maziko ya Padri Mushi

Padiri Mushi aliyeuawa kwa kupigwa risasi Jumapili iliyopita asubuhi wakati akishuka kutoka kwenye gari lake ili kwenda kuongoza ibada katika Kanisa la Betras, lililopo Minara Miwili, Mji Mkongwe, Unguja, anazikwa Jumatano wiki hii Visiwani humo.

Mazishi hayo yanafanyika jioni ya Jumatano hii katika Kijiji cha Kitope, Kaskazini B, Unguja yakiongozwa na Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Eusebius Nzingilwa.

Lakini kabla ya muda wa ibada hiyo ya mazishi, Kardinali Pengo ataongoza misa ya kumwombea marehemu pamoja na kuliombea Taifa itakayofanyika katika Kanisa Kuu Katoliki la Mtakatifu Joseph, jijini Dar es Salaam.

Masikitiko ya Rais Kikwete

Tayari Rais Jakaya Kikwete kupitia kwa Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu jijini Dar es Salaam, ameeleza kusikitishwa na tukio hilo na kuahidi serikali yake kuwasaka wote wanaohusika na kuwachukulia hatua za kisheria.

Hata hivyo, kauli hiyo ya Kikwete kupitia kwa Kurugenzi hiyo inatajwa na duru za baadhi ya viongozi wa dini nchini kuwa ni ya kawaida na imeanza kuzoeleka. Viongozi hao wanarejea ahadi yake aliyoitoa wakati Padri Ambrose Mkenda aliponusurika kuuawa huko Zanzibar, wakati wa Sikukuu ya Krismasi mwaka jana, na kuishia kujeruhiwa.

Lakini si padri huyo pekee aliyenusurika kuuawa bali vitendo vya kudhuru baadhi ya viongozi wa dini nchini pia vimemfika Sheikh Fadhil Suleiman Soraga, ambaye ni Katibu wa Mufti Zanzibar, ambaye alimwagiwa tindikali.

Hata hivyo, katika hatua nyingine tayari Serikali ya Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohammed Shein, nayo kama ilivyo kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano, imeahidi kuwasaka wahusika na kuwachukulia hatua.

Makanisa zaidi yacharuka

Hali imezidi kuwa tete ikiibua kauli na matamko mbalimbali ya viongozi wa dini nchini.

Jukwaa la Wakristo mkoani Mbeya ambalo linaundwa na mabaraza makuu matatu ya madhehebu ya kikristo; Tanzania Episcopal Council (TEC), Christian Council of Tanzania (CCT) na Pentecostal Council of Tanzania (PCT), limeitahadharisha serikali juu ya kile walichokiita undumilakuwili na tabia yake kulichukulia suala la mauaji ya viongozi wa dini ya Kikristo kama jambo la mazoea.

Jukwaa hilo, limesema katika tamko lake la wiki hii kwamba ili Serikali ya Rais Kikwete iweze kuaminika mbele ya macho ya waamini wa dini hiyo, lazima ionyeshe usawa katika sakata la mauaji ya Mchungaji Mathayo Kachila wa Buseresere, mkoani Geita na Padri Mushi wa Zanzibar.

“Miongoni mwa harakati hatarishi zinazosambazwa kwa njia ya CD na DVD ni za Sheikh (Hussein) Ilunga kuhusu kuuawa wachungaji, mapadri na maaskofu. CD na DVD zimeanza kuwa na matokeo mabaya kwani Padri (Ambrose) kule Zanzibar alipigwa risasi na watu walioitwa na Serikali wahuni, na sasa vifo vimetokea.

“Mchungaji Mathayo Kachila kule Buseresere mkoani Geita ameuawa na kikundi kinachodhaniwa ni wanaharakati wa kidini wenye jazba na ghadhabu kali inayotokana na mvutano uliopo kuhusu nani mwenye haki ya kuchinja wanyama, na juzi Padri Mushi wa Kanisa Katoliki kule Zanzibar,” alisema Askofu Damianus Kongoro wakati akisoma tamko la Jukwaa hilo mbele ya wandishi wa habari jijini Mbeya.

Mauaji kwingineko duniani

Mauaji ya mapdri yamewahi kutokea katika maeneo tofauti duniani na kati ya nchi ambako mauaji hayo yamepata kutokea ni Colombia.

Katika Jiji la Bogotá, Colombia, Kardinali Ruben Salazar aliwahi kuja juu dhidi ya mauaji ya Padri Luis Alfredo Suarez Salazar (50), akisema aliyeuawa hakuwa na hatia yoyote na wajibu wake ulikuwa ni mwema kwa jamii iliyokuwa ikimzunguka..

Padri huyo aliauwa kwa kupigwa risasi na watu wawili ambao baada ya tukio hilo walitoroka kwa kutumia pikipiki. Aliuawa wakati akimsaidia dada yake kupakia mizigo katika gari. Dereva wa padri huyo, Hernan Torres Ramos, naye alijeruhiwa vibaya.

Kutokana na tukio hilo, familia ya Padri Suarez ilieleza ya kwamba padri huyo hakuwa na kisasi na mtu yeyote na walishangazwa na mauji hayo, hali ambayo pia inafanana na maelezo ya wanafamilia wa Padri Mushi ambao kupitia kwa Aloyce Mushi aliyezungumza na mwandishi wetu anaeleza padri huyo naye hakuwa na kisasi na mtu au kundi lolote.

Mwanza balaa tupu

Kutoka mkoani Mwanza na Geita, Mwandishi Wetu anaripoti ya kwanza sakata la nani mwenye haki ya kuchinja wanyama katika Kijiji cha Buseresere-Geita, ambako Waziri Mkuu Mizengo Pinda alikwenda kutafuta suluhu, bado halijapata suluhisho.

Moja ya mambo yaliyoshuhudiwa na Waziri Mkuu Pinda katika ziara yake hiyo ni kuibuka kwa madai mapya ya kusambazwa biblia feki ambazo inadaiwa zinatumiwa na baadhi ya kundi lililoko kwenye mvutano huo kuthibitisha madai ya nani hasa mwenye mamlaka ya kuchinja kwa mujibu wa vitabu vyote vitakatifu vya Quraan na Biblia.

Katika kikao cha usuluhishi na Waziri Mkuu jijini Mwanza, inadaiwa ya kwamba Sheikh Issa Kalenga akiwa mmoja wa wajumbe wa mkutano huo alikuwa na biblia ambayo kwenye tafsiri ya maneno magumu imelieleza eneo kibudu kuwa ni mnyama aliyejifia mwenyewe au ambaye hakuchinjwa kwa mujibu wa taratibu za dini ya Kiislamu.

Taarifa zinaeleza kuwa biblia hiyo iliibua mjadala mzito kwa wachungaji kutoitambua na kumpelekea biblia nyingine tatu (Pinda) ili kuwaonyesha tafsiri hiyo lakini zikawa zimetofautiana.

Baada ya mkutano huo Shekh Kalenga waliowanyesha waandishi wa habari kipengele cha ufafanuzi huo na kusisitiza kuwa mkristu haruhusiwi kula kibudu na hivyo ni halali kula vilivyochinjwa na Waislamu.

Hata hivyo hoja hiyo ilipingwa na Askofu Augustine Mpemba wa Kanisa la TFE kwa Neema, ambaye alisema kuwa kuna watu wenye pesa ambao wamekuwa wakichapisha biblia zisizoendana na mafundisho ya Kikristo ili kuchakachua imani yao.

Alieleza kuwa katika ulimwengu wa leo kuna biblia nyingi sana wasizokubaliana nazo Wakristo, akitoka mfano wa Biblia ya John Hagee ambaye ni mwanzilishi wa Cornerstone Church, ambayo haikubaliki na Wakristu wengine kwa kuwa watu wanachapisha biblia hizo kwa maslahi, na kuwatahadharisha waumini wao kutonunua bila mitaani kwa kuwa ziko nyingi zilizochakachuliwa.

Lakini akizungumzia hali ya vurugu za kidini, mmoja wa wanazuoni wa Kiislamu alisema kwa jinsi matukio yalivyotokea (vurugu za uchinjaji na mauaji ya padri Zanzibar) inaashiria kuwa kuna watu mahali fulani ambao dhamira yao ni kuona Tanzania inaingia kwenye machafuko ili wao watimize malengo yao.

" Hii haiwezi kuwa imetokea kwa nasibu tu, kwamba Waziri Mkuu ana ratiba ya kukutana na viongozi wa dini zote halafu mtu anakwenda kumpiga risasi padri hadharani akijua wako waumini wanamsubiri kuwasuluhisha, huyu alidhamiria kutengeneza mshindo ambao utafanya mazungumzo yawe magumu," alieleza.

Alipoulizwa anadhani kuwa watu hao wanaweza kuwa nani na wanafanya hayo kwa manufaa gani alijibu; "Kwanza karibu asilimia kubwa ya biashara sasa zimeshikwa na bidhaa kutoka China, na hii ni kwa dunia nzima, mataifa makubwa ya Magharibi yamebakiza biashara ya maana ni silaha tu, wanaweza kuwa wanatafuta hilo soko Tanzania ambako kila kona imejaa dhahabu, gesi au mafuta na hivi vyote ni vivutio vya mataifa makubwa na China ndiyo wanaongeza ushawishi wao kwetu, mataifa makubwa yangependa kuona tunafarakana ili wapate fursa ya kunufaika kirahisi."
Share this article :

0 comments:

Speak up your mind

Tell us what you're thinking... !

ZILIZOSOMWA SANA.

Followers

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Proudly powered by Blogger
Copyright © 2011. Kitoloho - All Rights Reserved
Template Design by Creating Website Published by Mas Template