Mauwaji ya Alhaj Dr Jumbe IGP ategue kitendawili. - Kitoloho
Headlines News :
Home » » Mauwaji ya Alhaj Dr Jumbe IGP ategue kitendawili.

Mauwaji ya Alhaj Dr Jumbe IGP ategue kitendawili.

Written By Msamaa on Saturday, March 16, 2013 | 12:36 PM

Mauwaji ya Alhaj Dr Jumbe IGP ategue kitendawili.
 
DK. Jumbe Mohamed Maphingo alikufa Mei 23, 2011. Nilikuwa hoteli ya Bagamoyo Beach Resort na asubuhi sana baada ya swala ya alfajiri nilipata ujumbe wa simu ukisema kuwa Dk. Jumbe alikuwa ameuawa na kundi la wanafunzi Hospitali ya Kilutheri ya Bulongwa. Inasemekana wakati huo ilidaiwa kuwa ilikuwa ni kutokana na kujaribu kumbaka mwanafunzi wa kike! Nilishtuka kwani huyo asingeweza kuwa Jumbe niliyemfahamu. Nilimpigia simu aliyepeleka ujumbe huo na akanipa maelezo hayo hayo.

Jua lilipochomoza taarifa nyingine zikaibuka na wazi kabisa ungeweza kuanza kuona kuna zaidi ya kile kilichokuwa kinaelezwa kwa watu. Hata gazeti la Daily News la asubuhi hiyo lilichapisha habari hizo za jaribio la kubaka bila kuthibitisha kilichosemwa. Nilimwomba Mungu kuwa kama ukweli siyo huo, basi ukweli ufichuliwe.

Nani alikuwa Dk. Jumbe?
Dk. Jumbe alizaliwa na kukulia Pongwe, Tanga -kilomita chache kutoka mahali apozaliwa mama yangu lakini sikumfahamu hadi Mei 2009 tulipounda Mtandao wa Maendeleo wa Tawheed - kikundi ambacho kilikuwa na nia ya kuandaa safari za Hijja. Tulikuwa tunahitaji daktari na baadhi ya marafiki zangu wa karibu wakanielekeza kwa Dk. Junbe. Tulikwenda pamoja Makka mwaka ule na mahujaji 90. Kupunguza maelezo alikuwa kama mtu aliyevumbuliwa kwangu - alidhihirisha kuwa ni daktari hodari na aliyekubuhu,
lakini alikuwa zaidi ya hapo kwangu na kwa kikundi chetu.

Alikuwa anasaidia jikoni, kuleta vyakula kutoka madukani, alisaidia mahujaji wazee na takriban chochote kile ambacho kilihitaji kufanyika. Alikuwa mtu mtulivu na mshirika mahsusi wa shughuli za pamoja. Tulielewana papo kwa papo. Tuliporudi nyumbani tulikuwa karibu sana na nikaanza kumfahamu vyema zaidi na familia yake. Alikuwa rafiki mkubwa. Lakini alikuwa, kama nilivyogundua baadaye, rafiki wa karibu wa marafiki zangu wengi tu.

Baadaye akaniambia kuwa kuna shughuli anayoisimamia kule Iringa na alihitaji kusafiri kwenda kule mara kwa mara. Hakuniambia kuwa alikuwa amekubali ajira katika Hospitali ya Kilutheri ya Bulongwa. Nadhani alidhani ningemshauri vinginevyo lakini huo ulikuwa ni uamuzi wake.

Nini basi kilitokea?
Dk. Jumbe akiwa ni mtu wa jinsi alivyokuwa akidhihirisha sifa zake haraka sana. Alikuwa wakati wa kifo chake, nilivyoambiwa, Mnadhimu wa Chuo cha Tiba kilichounganishwa na hospitali hiyo. Usiku mmoja aliarifiwa kuwa mwanafunzi mmoja, wa kike alikuwa hajalala katika bweni. Aliagiza apewe maelezo ya maandishi kutoka kwa mwanafunzi huyo na hayakufika hadi usiku ambako aliuawa. Dk. Jumbe alikuwa akikaa katika nyumba ndani ya eneo la hospitali, peke yake. Mkewe na watoto walikuwa bado wanakaa Upanga, Dar es Salaam. Alikuwa na rafiki mwingine akiwa Bulongwa ambaye pia ni daktari na waliondoka pamoja kutoka Hospitali ya Muhimbili Dar es Salaam kwenda Bulongwa. Usiku wa mauaji yake daktari huyu alipigiwa simu na Dk, Junbe akimwambia kuwa kuna kundi la wanafunzi nje ya nyumba yake pamoja na huyo mwanafunzi wa kike aliyezungumziwa. Walikuwa wanaonekana kutaka kumshambulia, na ndiyo mara ya mwisho daktari huyo alisikia kutoka kwa Dk. Jumbe. Daktari huyo alikimbia kutoka Bulongwa na kuandika maelezo kwa Polisi Makao Makuu Dar es Salaam. Nilizungumza naye mimi binafsi pale Masjid Tambaza baada ya mazishi ya Dk. Jumbe.

Mwili wa Dk. Jumbe ulikutwa na majereha kichwani yaliyosababisha kifo chake muda mfupi baadaye nyumbani kwake. Nilielezwa kuwa mwili wa Dk. Jumbe ulikuwa unasafirishwa kwenda Tanga kwa njia ya barabara. Nilikuja Dar es Salaam nikaenda kwa ndege Tanga kupitia Zanzibar na Pemba na nikawahi kumzika rafiki yangu. Yalikuwa ni mauaji ya kikatili na nilikuwa natazamia kuwa Jeshi la Polisi litakamilisha uchunguzi huo. Hata kama Jeshi la Polisi halitafanya hivyo, kuna siku maalum ambako hukumu ya mwisho itafanyika. Takriban wiki mbili baada ya hapo sisi (Mtandao wa Maendeleo wa Tawheed) tuliamua kupeleka timu ya waandishi wa habari wawili na mpiga picha kwenda Bulongwa kuandika habari kuhusu kifo cha Dk. Jumbe. Walizungumza na maofisa na waliona ushahidi ulioachwa katika eneo la mauaji. Ilikuwa inashangaza kusikia kuwa bado kulikuwa na vifaa ilivyosemekana vilichukuliwa na kundi la wanafunzi ambavyo bado vilikuwa katika eneo hilo. Hivi Jeshi la Polisi linaweza kuruhusu uzembe kiasi hicho? Nilikataa kukubali hilo.

Lakini tulisikia kuwa watuhumiwa kadhaa walikuwa wamekamatwa na mara moja tukasikia kuwa kesi ya mauaji ilikuwa imefunguliwa na walikuwa wameshitakiwa. Kesi za mauaji huwa zinachukua muda mrefu na tulivuta subira. Jumapili (iliyopita) nilikutana na mjane wa Dk. Jumbe, nikiwa nimerudi Jumamosi usiku kutoka Cape Town (Afrika Kusini). Nilimbiwa kuwa alikuwa anahitaji sana kuniona. Tulikutana. Kumbe yeye na shemeji yake walitembelea Hospitali ya Kilutheri ya Bulongwa ili angalau kuona mahali mumewe alipofia na kupata habari kutoka kwa waliokuwepo, zaidi ya mwaka mmoja baada ya kifo chake kwa sababu hapakuwa na habari zozote zinazopatikana. Ndipo walipopata nakala ya ‘Nolle Prosequi’ kutoka kwa mkuu wa taasisi hiyo yenye tarehe Novemba 9, 2011 kuwaeleza kuwa Mkurugenzi wa Mashitaka (Serikalini) ameamua kutokuendesha kesi dhidi ya watuhumiwa. Ilikuwa ni mshtuko. Ingekuwaje jambo kama hilo litokee?

Mwaka mmoja uliopita na hakuna taarifa zilizotufikia? Unaweza kutetea hilo kwa njia gani? Ingewezekana vipi hilo litokee? Ni jinsi gani ambavyo mauaji yaliyofanywa na kundi la watu ambao waliacha mtiririko wa ushahidi wa maneno, vitu na vielelezo vya uchunguzi waishie kutokushitakiwa? Nini kilitokea? Hatuna majibu na kusema kweli nimepoteza imani kabisa sasa (na
vyombo vya dola). Nimepitia vianzio kadhaa na nina uhakika kuwa mauaji haya yangefunguliwa kesi kwa urahisi sana.

Ushahidi uko wapi?
Dk. Jumbe alizungumza na mfanyakazi mtaalamu mwenzake wakati alipoona hatari inamnyemelea -- usiku huo huo kabla ya kuuawa. Maelezo hayo walipewa Polisi kwa njia ya tarifa ya maandishi. Simu hiyo itakuwa imenakiliwa mahali na kilichomo kingechambuliwa kudhihirisha kilichotokea eneo hilo. Hiyo ilifanyika? Hiyo ingewapa Polisi kianzio kutoka kwa aliyeuliwa,
moja kwa moja. Nina uhakika kulikuwa na ushahidi mwingi tu katika eneo la mauaji. Katika mwili wa Dk. Jumbe na kuzunguka eneo hilo. Eneo la tukio la mauaji lilidhibitiwa ilivyopasa? Nina uhakika kulikuwa na majeraha, michubuko na bila shaka, damu. Kwa vile alipigwa mara nyingi na damu kuruka lazima itakuwa imewaangukia watu kadhaa kati ya kundi hilo.

Na vitasa vya milango, madirisha, n.k. Lazima kulikuwa angalau na alama za vidole kwa mbali katika vitu hivyo na vifaa vilivyoachwa katika eneo la mauaji. Kwa uchunguzi mzuri isingekuwa vigumu kuwafahamu waliokuwa hapo na walishika kitu gani. Vipi kuhusu kuwepo kwa vitu ambavyo havikuwepo wakati wa mauaji kwani watuhumiwa kadhaa, kwa kughafilika tu wakati huo, wataacha vifaa vya thamani kubwa kiushahidi, na hii inawezekana kabisa. Ingewezekanaje vitu kama hivi virukwe tu visiangaliwe? Ni kweli havikuangaliwa? Mwishowe, kundi la watu (kama ndivyo lilivyokuwa) la wanafunzi wa kiume na kike haliwezi tu kutoka katika
mabweni yao bila kuwepo maandalizi. Lazima kulikuwa na mawasiliano, ya mdomo, ya maandishi ya ujumbe wa simu au mazungumzo ya simu. Lazima
wangekuwepo na nina hakika bado wapo washuhuda wa kile kilichotokea kabla ya na baada ya mauaji. Na watu wanazungumza.

Wanaweza kufanywa wakaimba, licha ya kuzungumza. Vianzio vyote hivi havikusaidia kitu kweli? Siwezi kukubali kuwa hilo kabisa linawezekana. Tuliona wote jinsi Jeshi la Polisi linavyoweza kufanya kazi kwa bidii pale ofisa wa ngazi za juu wa Polisi, Mkuu wa Polisi mkoa wa Mwanza alipouawa usiku wa manane. Watuhumiwa wote walikamatwa na wamefunguliwa mashitaka. Mauaji ya Dk. Jumbe kwa kulinganisha yangekuwa ni rahisi zaidi kutatua na bado inawezekana.

Hatua nyingine?
Nitakuwa mwingi wa shukrani kwa Mkuu wetu wa Jeshi la Polisi kama angeulizia, yeye binafsi, kuhusu uchunguzi huo uliokwama. Kuna maelezo kuhusu mauaji ya Dk. Jumbe ambayo nisingependa kuingilia, lakini uchunguzi (wa kifo chake) unahitaji kurudiwa upya hasa kutoka Makao Makuu ya Jeshi la Polisi. Kama kuna gharama zinazohitaji kufikiwa, basi tufahamishwe na tutatoa kinachohitajika, kama Jeshi la Polisi haliwezi kufanya hivyo. Hata kama uchunguzi wa kimaabara unahitaji kufanyika.
Mwananchi mpenda haki
Share this article :

0 comments:

Speak up your mind

Tell us what you're thinking... !

ZILIZOSOMWA SANA.

Followers

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Proudly powered by Blogger
Copyright © 2011. Kitoloho - All Rights Reserved
Template Design by Creating Website Published by Mas Template