SHULE ZA MISHENI - Kitoloho
Headlines News :
Home » » SHULE ZA MISHENI

SHULE ZA MISHENI

Written By Msamaa on Sunday, June 9, 2013 | 12:37 PM

AN-NUUR
Na.153 Safar 1419, Juni 12-18, 1998
 
 
 

Hali ilivyokuwa kwenye shule za Misheni

Ni kwa muda mrefu kumekuwa na maelezo na malumbano mengi kuhusu suala la elimu na Waislamu wengi nchini mwetu kutopenda kutaka kusoma, pamoja na kuwepo shule nyingi zilizojengwa na kuendeshwa na makanisa katika kipindi cha ukoloni na mara baada ya uhuru (1961 - 1971). 
Mwandishi PILI SALUM anaelezea hali ilivyokuwa wakati huo kwenye shule hizo za Misheni katika makala hii. Endelea... 
Kutokana na ukanushwaji na upotoshwaji unaoendelea kutolewa na watu mbali mbali wa ngazi mbali mbali (rejea taarifa yya habari ya DTV ya tarehe juni 2, 1998 ya saa moja usiku) kuhusu uzembe wa Waislamu wengi kutopenda kusoma pamoja na mashirika mbali mbali ya kanisa kujenga na kuendesha shule hizo kwa wananchi wote bila upendeleo au masharti yoyote. 
Mimi nimeonelea leo nitumie fursa hii kutoa ushuhuda wangu kwa umma wa Tanzania nikiwa kama mmoja wa Waislamu niliobahatika kusoma kwenye shule hizo kuanzia darasa la pili hadi kidato cha nne (2-12) kati ya mwaka 1964-1973. 

Nitatumia fursa hii kueleza mazingira ya shule, kanuni na sheria za shule, taratibu za kila siku na mambo mengineyo yaliyokuwa yakijitokeza, na nitatoa mifano hai iliyotokea. Nia na lengo ni kutaka kumfanya kila msomaji aujue ukweli kuhusu shule hizo, kisha aweze yeye mwenyewe kupitisha hukumu kama kweli Waislamu walikataa kusoma kkwa uzembe au ni mazingira yaliwalazimisha kutokubali kwenda kusoma kwenye hizo shule.
Mazingira ya shule niliyosoma yalikuwa kwenye eneo la kanisa. Madarasa yote, mabweni na chumba cha chakula yalikuwa yamepambwa kwa sananu za Yesu akiwa msalabani. Picha hizi zilikuwa zimetundikwa juu ya ukuta mbele ya chumba. Mabweni yalikuwa na sanamu za watakatifu mbali mbali. Tulikuwa na Mt (St) Agnes, Mt Helen, Mt Mary, Mt Lucy, Mt Marietha. Hizi sanamu zilikuwa na ukubwa kwa kimo cha mtoto wa miaka 3/4 na zilikuwa chini na mbele ya chumba cha bweni.
Kulikuwa na bustani ndogo ambayo ilikuwa na pango dogo lenye sanamu nyingi mbali mbali, ikiwemo ya Yesu, mama wa Yesu Maria, Mt Joseph, Malaika na kondoo na mishumaa. Jirani ya shule kulikuwa na kijito kidogo kilichokuwa kinatoa maji kwa ajili ya matumizi mbali mbali ya kila siku ya wanafunzi, waalim, masista na mapadri. 

Kanuni na sheria za shule zilikuwa ni sawa kwa wanafunzi wote, bila kujali imani ya mwanafunzi. Kila siku asubuhi kabla ya masomo wanafunzi hujipanga mstari saa 1.00 asubuhi na hapo kiranja wa zamu hhutakiwa kuanzisha wimbo wa kwaya kufuatana na majilio (matukio ya kalenda ya kanisa) mathalani wakati wa kipindi cha Pentekoste au kwaresma, muimbishaji hutakiwa kuimba mwimbo unaohusiana na hali ya kipindi hicho. Kwa mfano wimbo huu "UJE ROHO MUUMBAJI UTAKASE NYOYO ZETU...." 

Hapo suala la dini ya mtu hakuna kuangaliwa, hivyo wanafunzi wote tuliitikia. Baada ya hapo tuliingia darasani na huko kiranja wa darasa alianzisha sala kabla ya kuanza kusoma kwa kusema kwa sauti kuwa "Kwa jina la Baba, na la Mwana na la Roho Mtakatifu", kisha ikafuatia na Salam Maria na Baba yetu Uliye Mbinguni. Haya tulisoma wote kwa sauti kubwa bila ya kujali dini ya mtu. Saa nne tulikwenda chumba cha chakula na kiranja wa chakula alianzisha sala ya BABA YETU kwa sauti na sote tuliitikia kisha tulikaa chini na kunywa uji. Tulirejea madarasani na vipindi viliendelea mpaka saa 6.30 kengele ya kanisa inalia ambayo tuliita ANJELUSI na ni lazima kila mtu asimame na kutulia alipo mpaka itakaponyamaza, kisha hufuatiwa na sala fupi na ndipo vipindi huendelea tena. Hii ni kila siku na hufanyika hivyo mahali popote utakapokuwepo hata kama unakula inabidi uache kwanza na kutekeleza ibada hiyo.Vipindi vikimalizika jioni tunafanya kazi za shamba, mikono na usafi mpaka saa 11.30 ndipo kenglele ya shule hugongwa na kuamuriwa wote kwenda pangoni kwa ibada. Hapo hakuna cha imani ya mtu. Tunapiga magoti mbele ya pango na kusali.
Baada ya kujisomea usiku saa 3.00 wanafunzi tulienda mabwenini kwetu na kabla ya kkulala tulipiga magoti mbele ya sanamu la bweni na kiranja alianzisha sala kwa kusoma SALAAM MARIA na BABA YETU ULIYE MBINGUNI, KISHA kisha tuliruhusiwa kulala. Hiyo ndiyo taratibu ya maisha ya kila siku unaingia shule mpaka unapomaliza shule.Zaidi ya hapo kuna vipindi vya kusali ROZALI, vipindi vya shida mbali mbali ambazo ibada hufanyika kwa pamoja bila kujali imani ya mtu. Kutokana na hali hii kila mwanafunzi ni lazima afahamu vyema sala na nyimbo hizo.
Siku za jumapili na siku za kanisa kama Pasaka, X-mas, kupaa Rabi mbinguni na za watakatifu mbali mbali wakrisoto huenda Kanisani na ni siku ya neema kwa wanafunzi kwani chai na mikate hun ywewa na wali kwa nyama huliwa.
Mwezi wa Ramadhan ni marufuku kwa mwanafunzi wa Kiislamu kufunga (kosa) hivyo tulikuwa hatufungi wala hakuna cha sala ya Ijumaa au Idd. Siku za Jumamosi tulifanya usafi hivyo wanafunzi walichaguliwa kumsaidia Sista wa Kanisa kuandaa kwa ajili ya Misa ya Jumapili kama kuiandaa ARTARE, vikombe vya divai, SAKRAMENTI. Yoyote alichaguliwa bila kujali imani yake.  

Shuleni walikuwa wanafuga nguruwe ambao walihudumiwa na wafanyakazi. Wakati wa kuchinja ukifika huchinjwa na utumbo huenda kuoshewa mtoni ambako ndiko maji yake hutumika shuleni. Maji hayo huvutwa na pampu mpaka kwenye tanki, pampu hiyo iko upande wa chini ya mto, na waoshaji nyama hizo upande wa juu wa mto hivyo kufanya mafuta na vipande vya nyama kuingia kwenye tanki la maji. Nyama hugawiwa nyingine kwa wanafunzi na kupelekwa jikoni ambako hupikwa pamoja na nyama ya ng'ombe. Siku hiyo huwa ni ngumu kwa wanafunzi wa Kiislamu kwani wengine hugomea kula chakula hicho. Lakini maji, vyombo vyote tayari vinanajisi. Na hiyo ni ya kudumu kwani najisi imeenea kote.Waalimu, wafanyakazi wote wa shule walikuwa ni Wakristo na shule ilikuwa ni ya bweni iliyo mbali na kijiji hivyo malezi yote ya wanafunzi yalikuwa kwa misingi ya Kanisa. Nakumbuka mara kadhaa kati ya mwaka 1964-1966 mwalimu mkuu alipokuwa anapenda kuwauliza wanafunzi mstarini asubuhi "ni dini gani Waumini wake ni maskini?" Wanafunzi tuliambiwa kujibu "Waislamu". Mwalimu huuliza tena "ni dini gani Waumini wake wanavaa viraka? Tunajibu Waislamu. Kisha huuliza " ni dini gani waumini wake wanavaa Suti? Hujibiwa WAKRISTO. Hapo hutuambia tumejibu vyema na kuturuhusu kuingia madarasani.
Ndugu msomaji hayo ndiyo baadhi ya mambo yaliyokuwa yakitendeka kwenye mojawapo ya shule hizo tunazoambiwa Waislamu tulikataa kwenda kusoma kwa uzembe wetu. 

Tukirudi likizo ukithubutu kusimulia mikasa hiyo mzazi anahamaki na kukutaka usirudi tena shuleni kutokana na mambo yanayotendeka kuwa kinyume na Uislamu. Mimi binafsi nilimaliza kusoma baada ya baba yangu kuamua nisome tu hivyo hivyo lakini nikimaliza nisilimishwe upya kwani aliamini kabisa kwamba isikuwa tena Muislamu kutokana na tuliyokuwa tunayatenda hshuleni. Hebu ndugu msomaji fikiria mtoto wa miaka kati ya 7-15 awe katika maisha haya unategemea atakuwa muumini kweli wa Uislamu au Ukristo? Hivyo tulipata kazi baada ya kumaliza shule, tuanze kufundishwa Uislamu pamoja na kubahatika kuzaliwa kwenye familia za Kiislamu. 

Katika kipindi hicho baadhi wanafunzi waliamua kubatizwa baada ya kuvutiwa na mambo ya kanisani kutokana na nyimbo na sherehe mbalimbali za kanisa. Pia baadhi ya walio na umri mkubwa kiasi waliacha shule kati ya darasa la 3-4 kutokana na kuelewa nini kinachotendeka na kuchoka kusikia Uislamu ukitukanwa kila siku hapo shuleni.Kwa muhtasari huo wa mambo yaliyokuwa yakitendeka kwenye shule ambayo mimi mwenyewe nimezisoma kati ya mwaka 1964-1973, ndugu msomaji utawahukumu ivipi Waislamu. Walikuwa wazembe hawakutaka kusoma, au wenye shule walikuwa wanawatoa Waislamu wasisome kwenye shule zao?"Akukataae hakuambii toka ila utaona mamboye yanavyokwenda": Hii ni methali ya kiswahili yenye maana, usisubiri kauli ya kufukuzwa ila utumie hekima zako na busara kuondoka kutokana na vitendo unavyotendewa. 

Suala la imani ni zito, hivyo kutuambia tulikataa shule wakati mazingira yote yalikuwa yanamkataa Muislamu, ni kuudanganya umma na kuukataa ukweli wa kihistoria ambao uko wazi kabisa. Hii ni sawa na kisa cha Adili na Nduguze katika kitabu cha marehemu Shaaban Robert, kilichoelezea kisa cha Adili cha kuwatandika bakora nduguze mpaka wazimie, wakisha zinduka anawaandalia chakula kizuri na kula nao mezani. Lakini, kwa kuwa Adili alifanya hivyo kwa kulazimishwa, na pia alijua kufanya hivyo ni kuwatesa (manyani) hao nduguze, ndiyo maana kila ulipowadia wakati huo alilia sana kwa uchungu kuonyesha kuwa si haki na wala si halali kumtandika mtu kisha umpe chakula. 

Ni bora usimpe kabisa kuliko kudanganya unampenda na kumpa chakula kizuri wakaiti unamtesa. Ndiyo maana mgeni wa Adili alishangaa na kushindwa kumuelewa na hivyo kuchukuwa hatuwa ya kuitoa hiyo siri kwa kiongozi wa nchi. Pia hali kadhalika haikuwa halali kutoa elimu hizo kwa misingi hiyo iliyokuwa natendeka. Imani ya mwanafunzi ilipasa kuheshimiwa na kuthaminiwa. 
Share this article :

0 comments:

Speak up your mind

Tell us what you're thinking... !

ZILIZOSOMWA SANA.

Followers

Blog Archive

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Proudly powered by Blogger
Copyright © 2011. Kitoloho - All Rights Reserved
Template Design by Creating Website Published by Mas Template