- Kitoloho
Headlines News :
Home » »

Written By Msamaa on Thursday, June 27, 2013 | 12:21 PM

ISHARA ZA MAUAJI YA KIMBARI ZI WAZI TANZANIA; KIJO-BISIMBA

Dr-Helen-Kijo-Bisimba 

Tanzania imekuwa ikijulikana kama kisiwa cha amani na hivyo kuwa kimbilio la wakimbizi kutoka nchi jirani. Hata hivyo kwa takribani miaka mitatu tumeshuhudia amani hiyo ikitoweka kwa kuwepo matukio mbalimbali yanayohusiana na itikadi za kidini yanayojenga mazingira ya kutokea kwa mauaji ya halaiki (mass killings) au ya kimbari (genocide). Kwa muda mrefu, Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kimekuwa kikifuatilia hali ya kuendelea kupungua kwa uvumilivu (tolerance) baina ya vikundi vyenye misimamo tofauti ya kisiasa au vile vinavyotofautiana kwa imani za dini. Kupungua kwa uvumilivu wa kisiasa kulianza mwishoni mwa miaka ya 1990 na kwa wakati huo hali ilikuwa tete zaidi kwa upande wa Tanzania Zanzibar. Kwa upande wa Tanzania bara hali hiyo ilikuwa ikijitokeza zaidi wakati wa chaguzi ndogo. Kwa ujumla uvumilivu wa kidini haukutetereka sana kama ulivyokuwa uvumilivu wa kisiasa. Hata hivyo, hali ya kupungua kwa uvumilivu wa kidini ilianza kujitokeza kwa kasi zaidi kwenye kampeni za uchaguzi wa mwaka 2010 wakati ambapo baadhi ya wanasiasa walitumia dini kama kiungo cha kupata madaraka na kuweka mambo mbalimbali yanayohusiana na dini kwenye ilani za uchaguzi. Aidha wakati huohuo viongozi tofauti wa kidini walitoa matamko kadha wa kadha kuhusiana na mustakabali wa taifa.

Mara baada ya uchaguzi huo, tulishuhudia baadhi ya taasisi za dini zikiitisha makongamano kujadili masuala mbalimbali ya kisiasa. Mengine yakiendelea kuonesha kutoridhishwa na muelekeo wa maendeleo ya taifa na mengine yakikejeli au kujaribu kutoa majibu kwa makongamano menza ya dini kwa kuutetea mfumo uliopo. Aidha yapo makongamano mengine yaliyokwenda mbali zaidi na kuanza kushutumu kuwa nchi ya Tanzania inaendeshwa kwa ‘mfumo kristo’. Kwa sababu hiyo kumekuwa na vipeperushi, kanda, makongamano kuzunguka mikoa yote ya Tanzania, vipindi vya radio na magazeti yakitoa kauli zinazojenga chuki za kidini miongoni mwa wananchi wa Tanzania. Pamoja na harakati zote hizo, Kituo kilishtushwa kwa kuona kuwa hakukuwa na hatua madhubuti zilizochukuliwa na serikali ili kuzuia kuendelea kujenga chuki za kidini. Matokeo yake Tanzania ilishuhudia kuchomwa kwa Makanisa, kuharibiwa kwa mali mbalimbali, kuumizwa kwa watu mbalimbali na hata kuuwawa kwa viongozi wa dini. Kwa muhtasari – tangu mwaka 2010 Kituo kimeweka kumbukumbu ya matukio kumi na tisa (19) yanayohusiana na vurugu za kidini na hakuna hatua yoyote makini inayochukuliwa na vyombo husika kuzuia hali hii.

Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu kinahofu kuwa, ikiwa hali hii ikiachwa bila udhibiti inaweza kabisa kulifikisha taifa katika mauwaji ya halaiki, vita ya wenyewe kwa wenyewe au hata mauaji ya kimbari. Kitaalam mauaji ya kimbari huweza kupitia katika hatua nane, na ya kwanza ni Ubaguzi (classification) ambao watu hujiita sisi dhidi ya wao na kuanza kuwatenga wale walio tofauti. Kwa mfano kabila dhidi ya kabila na dini dhidi ya dini (ukristo dhidi ya uislam. Pili ni kutoa majina au alama (symblolization) ambazo huonyesha chuki dhahiri na kuwaita majina mabaya waliotofauti. Ukifuatilia kwa kina vipeperushi, jumbe katika mikutano na kanda utaona majina mbalimbali wanayopewa waumini wa dini ya kikristo dhidi ya waislam [kwa mfano Makafiri]. Hatua ya tatu ni udhalilishaji (dehumanization) ambapo mhusika huwaondolea heshma ya utu wale wote wanaotofautina naye na kuwaweka kwenye daraja la chini kama vile ni viumbe duni wasio na hadhi ya ubinadamu. Katika hatua hii, kundi fulani huhesabu kuwa dini/imani/dhehebu/itikadi yao fulani ni bora kuliko nyingine hivyo kuanza kuwadhalilisha wote wasiokuwa wa dini/imani/dhehebu/itikadi yao. Hatua ya nne ni kujiunga pamoja au kujiratibu (mobilization) kwa kuanza kuandaa mipango, kutoa mafunzo ya chuki na kubuniwa mbinu na hatua mbalimbali za kuchukuwa dhidi ya watu waliotofauti. Tano ni mgawanyiko/kambi mbili (polarization) ambapo kauli za kuchochea chuki na propaganda kusambazwa. Hatua ya sita maandalizi (preparation) kuwatambua rasmi watu tofauti na kuwatendea kama adui na kuwajengea mazingira ya kuwashambulia. Hapa watu wanatayarisha silaha, wapiganaji wa kichinichini kama tunavyosikia huko ukerewe na sehemu zingine ambazo hatujazijua bado. Hatua ya saba maangamizi (extermination) ambayo ni mauaji yaliyoratibiwa na kufanyika mfululizo kwa utaratibu maalum dhidi ya kundi moja. Ikiwa katika hatua hii mauaji hayo yatafanikiwa ndiyo huitwa mauaji ya kimbari(genocide) na ikiwa walengwa wataamua kupambana ndipo hutokea mapigano ya wenyewe kwa wenyewe (civil war). Hatua ya mwisho ni kukanusha (denial). Katika hatua hii, mara zote wauaji na vizazi vyao vilivyopo na vitakavyokuja mara zote hujitahidi kukanuasha kuwa hayo hayakuwa mauaji ya kimbari ila ilikuwa ni kulipiza kisasi, kusafisha jamii dhidi ya uchafu, kuadhibu waasi, au kuwaondoa vibaraka.

Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu, baada ya kufanya ufuatiliaji wa karibu na kuweka kumbukumbu ya matukio mbalimbali ya nayohusiana na kukosekana kwa uvumilivu wa kidini, kinatoa wito ufuatao kwa Seikali, taasisi za kidini na wananchi: Serikali:
i) Serikali ichukue hatua za haki na za dhati katika kuwakamata na kuwafungulia mashtaka wale wote wanaohusika na harakati za kuondoa uvumilivu wa kidini katika nchi yetu
ii) Serikali ihusike katika kupiga marufuku vyombo vya habari, mikutano na matangazo yote yanayoeneza chuki, ikiwa ni pamoja na kuondoa vipeperushi, kanda na nyaraka zozote yanayochochea chuki na zinazohatarisha taifa kutumbukia katika mauaji ya kimbari
iii) Serikali isimamie sheria na katiba ya nchi kuhakikisha kuwa uhuru wa kuabudu pamoja na uhuru wa maoni hautumiwi vibaya na kuhatarisha usalama wa taifa na watu wake.
iv) Serikali ishughulikie kero za watanzania waliowengi ambao huweza kusadiki propaganda yoyote kutokana na wingi wa mahitaji yao ya kila siku kama elimu, afya, maji, chakula, ajira na malazi.

Taasisi za Dini:
i) Kila taasisi ya kidini iheshimu ibara ya 19 ya Katiba ya nchi inayotoa uhuru wa kuabudu dini tunayoitaka na kuheshimu imani za wengine.
ii) Viongozi wa dini waweke mkazo na kuwahimiza waumini wao kuhusu umuhimu wa uvumilivu wa imani tofauti kama moja wapo ya nguzo kuu za amani ya taifa.
iii) Viongozi wakuu wa dini, wakaripie na kuwachukulia hatua wenzao wanaotoa kauli zinazoashiria chuki na uvunjifu wa amani

Wananchi:
i) Wananchi wa Tanzania tukatae kutumiwa na wanasiasa au viongozi wa dini wanaotuhamasisha kugombana baina yetu kwa misingi ya dini
ii) Wananchi tuendeleze amani ya taifa letu kwa kuheshimu imani ya kila mmoja ili kuliepusha taifa na mauaji ya kimbari au vita vya wenyewe kwa wenyewe ambavyo vitatuongezea zaidi shida kuliko kutatua matatizo tuliyonayo
iii) Wananchi tuchukue hatua ya kutoa taarifa kwenye vyombo vya usalama pale watu wanapotoa kauli na propaganda zinazochochea chuki miongoni mwa jamii

Imetolewa na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu
Dr.Helen Kijo-Bisimba,
Mkurugenzi Mtendaji.

 http://community.co.tz/2013/03/20/ishara-za-mauaji-ya-kimbari-zi-wazi-tanzania-kijo-bisimba/

Share this article :

0 comments:

Speak up your mind

Tell us what you're thinking... !

ZILIZOSOMWA SANA.

Followers

Blog Archive

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Proudly powered by Blogger
Copyright © 2011. Kitoloho - All Rights Reserved
Template Design by Creating Website Published by Mas Template