Sumaye amponda Lowassa. - Kitoloho
Headlines News :
Home » » Sumaye amponda Lowassa.

Sumaye amponda Lowassa.

Written By Msamaa on Monday, June 24, 2013 | 11:28 AM



TANZANIA DAIMA: 24 Juni 2013.
na Mwandishi wetu

WAZIRI Mkuu mstaafu Frederick Sumaye amesema anashangazwa na baadhi ya viongozi wa dini kutoa sifa nzuri kwa watu wanaochanga fedha na si kuzingatia uadilifu na wema walionao.
Kiongozi huyo alitoa kauli hiyo jana katika sherehe za kutimiza miaka 50 tangu kuanzishwa kwa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), zilizofanyika katika Chuo Kikuu cha Makumira mkoani Arusha.
Sumaye alihoji kuwa inakuwaje wema wa baadhi ya watu unajitokeza zaidi wakati nchi ikielekea kwenye uchaguzi unaotegemewa kufanyika mwaka 2015.
Sherehe hizo za kutimiza miaka 50 zilifanyika katika Chuo Kikuu cha Makumira na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wa KKKT kutoka sehemu mbalimbali duniani pamoja na maaskofu wote wa dayosisi 20 zilizopo nchini.
Ingawa Sumaye hakumtaja anayemlenga, lakini inaonekana kumlenga Waziri Mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa ambaye katika siku za hivi karibuni amekuwa akimiminiwa sifa kuwa ni mpambanaji wa umasikini na mtu mzuri katika kuendesha  harambee makanisani zinazowezesha kupatikana mamilioni ya fedha.
Hivi sasa, Lowassa anaonekana ndiye ‘mtaji’ mkubwa kwa viongozi wa makanisa yanayohitaji kuendeleza miradi mbalimbali ambapo wamekuwa wakimualika kwenye harambee zao.
Lowassa mwenyewe alikaririwa hivi karibuni mkoani Dodoma akisema kuwa yeye hana mamilioni ya fedha kama baadhi ya watu wanavyomhusisha anaposhiriki harambee, bali ana watu wenye ushawishi katika jamii.

Kauli ya Sumaye
Sumaye alisema ni jambo la kutia aibu na kushtua kuona watu wakipewa sifa za kuvutia kwa sababu ya kuchangia mamilioni kwenye shughuli za kanisa au binafsi na si kwa sababu ya uadilifu au wema wao.
Alisema katika siku za hivi karibuni kumeibuka mambo mengi machafu yaliyokithiri katika jamii na watu wanyonge kukosa haki zao za msingi hadi watoe hongo au rushwa.
“Nafasi katika nchi zimekuwa za biashara, watu hawaangalii tena uwezo au uadilifu wa mtu anayeutaka uongozi bali wanaangalia ametoa fedha kiasi gani za kuwahonga wapiga kura.
“Hata katika baadhi ya dayosisi zetu na sharika zetu watu wakipewa sifa za ajabu si kwa sababu ya uadilifu wao au wema wao, bali kwa sababu tu wamechangia fedha kwa shughuli zetu za kanisa au hata binafsi.
“Hatujiulizi kuwa mbona wema huu unajitokeza zaidi wakati kama kuna uchaguzi unaotegemewa? Je, hapo hatusatahili kutupwa nje na kukanyagwa kanyagwa kwa sababu chumvi imepotea utamu wake?
“Je, haya ni mafanikio ya miaka 50 ya kanisa au ni maeneo ambayo inabidi tujitazame na tujirekebishe?” alihoji.
Kuhusu kanisa hususani masuala ya kijamii, Sumaye alisema pamoja kushughulikia masuala ya kiroho, bado linapaswa kushughulikia masuala ya mwili ambao ni hekalu la Mungu, hivyo kanisa lina jukumu kujenga jamii yenye maadili mema na kukemea maadili mabaya.
“Yesu alisema; ‘nyinyi ni chumvi ya ulimwengu’, lakini chumvi ikiwa imeharibika itatiwa nini hata ikolee? Haifai tena ni ya kutupwa nje ikinyagwe na watu.

“Lakini nasema nyinyi ni nuru ya ulimwengu, hivyo ni wajibu wenu kutoa nuru kwa wengine maana yake ni kutoa malezi mema kwa jamii. Je, kanisa letu limefanikiwa kwa kiasi gani katika eneo hili?
“Je, tumekuwa na ujasiri wa kukemea mabaya hata kama kukemea huko kunawaudhi au kuwakera wenye mamlaka au na wenye nguvu za fedha? Je, tuna ujasiri kama wa Nabii Mikaya mwana Imla, aliyemwambia mfalme wake nitasema yake bwana aliyoniambia na kumwambia mfalme kuwa ukienda kupigana vita vya kuteka Tamoth Gileadi hutarudi hai?” alihoji Sumaye.
Sumaye pia alizungumzia matukio yaliyoanza kujitokeza katika siku za hivi karibuni akisema hivi sasa taifa limekuwa na matatizo mengi ya watu kuchukiana kwa sababu ya imani zao, mabomu kulipuliwa katika mikusanyiko ya jamii na kuteketeza watu wasio na hatia.
“Leo Watanzania wanabaguana kwa maeneo wanakotoka na sababu nyingine zisizo na msingi, matukio ya viongozi wa dini kuuawa, uchomaji moto wa makanisa, mapigano ya nani achinje mnyama, haya yote ni mambo mageni nchini mwetu, tuendelee kuimboea nchi yetu amani, lakini wakati maombi yakiendelea Watanzania tujue tunajichimbia kaburi letu wenyewe kama hatutapiga vita maovu haya,” alisema Sumaye.
Naye Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri nchini, Askofu Dk. Alex Malasusa, alisema kanisa halitaogopa hujuma au kusema ukweli na wataendelea kujenga marafiki wema bila kujali itikadi za marafiki wao.
Katika hatua nyingine, Askofu Malasusa alibainisha kuwa kitendo cha viongozi dini ya Kiislamu kuhudhuria sherehe hizo za miaka 50 kimeonyesha sura mpya.

“Kuwapo kwa viongozi wa dini ya Kiislamu kumedhihirisha kuwa yanayozungumzwa nje si halisi,” alisema Dk. Malasusa.
Katika sherehe hizo maaskofu wa kanisa hilo walihudhuria ikiwamo pia viongozi kutoka sehemu mbalimbali duniani.
Share this article :

0 comments:

Speak up your mind

Tell us what you're thinking... !

ZILIZOSOMWA SANA.

Followers

Blog Archive

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Proudly powered by Blogger
Copyright © 2011. Kitoloho - All Rights Reserved
Template Design by Creating Website Published by Mas Template