Tanzania
imekuwa ikijulikana kama kisiwa cha amani na hivyo kuwa kimbilio la
wakimbizi kutoka nchi jirani. Hata hivyo kwa takribani miaka mitatu
tumeshuhudia amani hiyo ikitoweka kwa kuwepo matukio mbalimbali
yanayohusiana na itikadi za kidini yanayojenga mazingira ya kutokea kwa
mauaji ya halaiki (mass killings) au ya kimbari (genocide). Kwa muda
mrefu, Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kimekuwa kikifuatilia
hali ya kuendelea kupungua kwa uvumilivu (tolerance) baina ya vikundi
vyenye misimamo tofauti ya kisiasa au vile vinavyotofautiana kwa imani
za dini. Kupungua kwa uvumilivu wa kisiasa kulianza mwishoni mwa miaka
ya 1990 na kwa wakati huo hali ilikuwa tete zaidi kwa upande wa Tanzania
Zanzibar. Kwa upande wa Tanzania bara hali hiyo ilikuwa ikijitokeza
zaidi wakati wa chaguzi ndogo. Kwa ujumla uvumilivu wa kidini
haukutetereka sana kama ulivyokuwa uvumilivu wa kisiasa. Hata hivyo,
hali ya kupungua kwa uvumilivu wa kidini ilianza kujitokeza kwa kasi
zaidi kwenye kampeni za uchaguzi wa mwaka 2010 wakati ambapo baadhi ya
wanasiasa walitumia dini kama kiungo cha kupata madaraka na kuweka mambo
mbalimbali yanayohusiana na dini kwenye ilani za uchaguzi. Aidha wakati
huohuo viongozi tofauti wa kidini walitoa matamko kadha wa kadha
kuhusiana na mustakabali wa taifa.
Mara baada ya uchaguzi huo, tulishuhudia
baadhi ya taasisi za dini zikiitisha makongamano kujadili masuala
mbalimbali ya kisiasa. Mengine yakiendelea kuonesha kutoridhishwa na
muelekeo wa maendeleo ya taifa na mengine yakikejeli au kujaribu kutoa
majibu kwa makongamano menza ya dini kwa kuutetea mfumo uliopo. Aidha
yapo makongamano mengine yaliyokwenda mbali zaidi na kuanza kushutumu
kuwa nchi ya Tanzania inaendeshwa kwa ‘mfumo kristo’. Kwa sababu hiyo
kumekuwa na vipeperushi, kanda, makongamano kuzunguka mikoa yote ya
Tanzania, vipindi vya radio na magazeti yakitoa kauli zinazojenga chuki
za kidini miongoni mwa wananchi wa Tanzania. Pamoja na harakati zote
hizo, Kituo kilishtushwa kwa kuona kuwa hakukuwa na hatua madhubuti
zilizochukuliwa na serikali ili kuzuia kuendelea kujenga chuki za
kidini. Matokeo yake Tanzania ilishuhudia kuchomwa kwa Makanisa,
kuharibiwa kwa mali mbalimbali, kuumizwa kwa watu mbalimbali na hata
kuuwawa kwa viongozi wa dini. Kwa muhtasari – tangu mwaka 2010 Kituo
kimeweka kumbukumbu ya matukio kumi na tisa (19) yanayohusiana na vurugu
za kidini na hakuna hatua yoyote makini inayochukuliwa na vyombo husika
kuzuia hali hii.
Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu
kinahofu kuwa, ikiwa hali hii ikiachwa bila udhibiti inaweza kabisa
kulifikisha taifa katika mauwaji ya halaiki, vita ya wenyewe kwa wenyewe
au hata mauaji ya kimbari. Kitaalam mauaji ya kimbari huweza kupitia
katika hatua nane, na ya kwanza ni Ubaguzi (classification) ambao watu
hujiita sisi dhidi ya wao na kuanza kuwatenga wale walio tofauti. Kwa
mfano kabila dhidi ya kabila na dini dhidi ya dini (ukristo dhidi ya
uislam. Pili ni kutoa majina au alama (symblolization) ambazo huonyesha
chuki dhahiri na kuwaita majina mabaya waliotofauti. Ukifuatilia kwa
kina vipeperushi, jumbe katika mikutano na kanda utaona majina
mbalimbali wanayopewa waumini wa dini ya kikristo dhidi ya waislam [kwa
mfano Makafiri]. Hatua ya tatu ni udhalilishaji (dehumanization) ambapo
mhusika huwaondolea heshma ya utu wale wote wanaotofautina naye na
kuwaweka kwenye daraja la chini kama vile ni viumbe duni wasio na hadhi
ya ubinadamu. Katika hatua hii, kundi fulani huhesabu kuwa
dini/imani/dhehebu/itikadi yao fulani ni bora kuliko nyingine hivyo
kuanza kuwadhalilisha wote wasiokuwa wa dini/imani/dhehebu/itikadi yao.
Hatua ya nne ni kujiunga pamoja au kujiratibu (mobilization) kwa kuanza
kuandaa mipango, kutoa mafunzo ya chuki na kubuniwa mbinu na hatua
mbalimbali za kuchukuwa dhidi ya watu waliotofauti. Tano ni
mgawanyiko/kambi mbili (polarization) ambapo kauli za kuchochea chuki na
propaganda kusambazwa. Hatua ya sita maandalizi (preparation)
kuwatambua rasmi watu tofauti na kuwatendea kama adui na kuwajengea
mazingira ya kuwashambulia. Hapa watu wanatayarisha silaha, wapiganaji
wa kichinichini kama tunavyosikia huko ukerewe na sehemu zingine ambazo
hatujazijua bado. Hatua ya saba maangamizi (extermination) ambayo ni
mauaji yaliyoratibiwa na kufanyika mfululizo kwa utaratibu maalum dhidi
ya kundi moja. Ikiwa katika hatua hii mauaji hayo yatafanikiwa ndiyo
huitwa mauaji ya kimbari(genocide) na ikiwa walengwa wataamua kupambana
ndipo hutokea mapigano ya wenyewe kwa wenyewe (civil war). Hatua ya
mwisho ni kukanusha (denial). Katika hatua hii, mara zote wauaji na
vizazi vyao vilivyopo na vitakavyokuja mara zote hujitahidi kukanuasha
kuwa hayo hayakuwa mauaji ya kimbari ila ilikuwa ni kulipiza kisasi,
kusafisha jamii dhidi ya uchafu, kuadhibu waasi, au kuwaondoa vibaraka.
Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu,
baada ya kufanya ufuatiliaji wa karibu na kuweka kumbukumbu ya matukio
mbalimbali ya nayohusiana na kukosekana kwa uvumilivu wa kidini, kinatoa
wito ufuatao kwa Seikali, taasisi za kidini na wananchi:
Serikali: i) Serikali ichukue hatua za haki na za dhati katika kuwakamata na
kuwafungulia mashtaka wale wote wanaohusika na harakati za kuondoa
uvumilivu wa kidini katika nchi yetu
ii) Serikali ihusike katika kupiga marufuku vyombo vya habari, mikutano
na matangazo yote yanayoeneza chuki, ikiwa ni pamoja na kuondoa
vipeperushi, kanda na nyaraka zozote yanayochochea chuki na
zinazohatarisha taifa kutumbukia katika mauaji ya kimbari
iii) Serikali isimamie sheria na katiba ya nchi kuhakikisha kuwa uhuru
wa kuabudu pamoja na uhuru wa maoni hautumiwi vibaya na kuhatarisha
usalama wa taifa na watu wake.
iv) Serikali ishughulikie kero za watanzania waliowengi ambao huweza
kusadiki propaganda yoyote kutokana na wingi wa mahitaji yao ya kila
siku kama elimu, afya, maji, chakula, ajira na malazi.
Taasisi za Dini: i) Kila taasisi ya kidini iheshimu ibara ya 19 ya Katiba ya nchi
inayotoa uhuru wa kuabudu dini tunayoitaka na kuheshimu imani za
wengine.
ii) Viongozi wa dini waweke mkazo na kuwahimiza waumini wao kuhusu
umuhimu wa uvumilivu wa imani tofauti kama moja wapo ya nguzo kuu za
amani ya taifa.
iii) Viongozi wakuu wa dini, wakaripie na kuwachukulia hatua wenzao wanaotoa kauli zinazoashiria chuki na uvunjifu wa amani Wananchi: i) Wananchi wa Tanzania tukatae kutumiwa na wanasiasa au viongozi wa
dini wanaotuhamasisha kugombana baina yetu kwa misingi ya dini
ii) Wananchi tuendeleze amani ya taifa letu kwa kuheshimu imani ya kila
mmoja ili kuliepusha taifa na mauaji ya kimbari au vita vya wenyewe kwa
wenyewe ambavyo vitatuongezea zaidi shida kuliko kutatua matatizo
tuliyonayo
iii) Wananchi tuchukue hatua ya kutoa taarifa kwenye vyombo vya usalama
pale watu wanapotoa kauli na propaganda zinazochochea chuki miongoni mwa
jamii
Imetolewa na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu Dr.Helen Kijo-Bisimba,
Mkurugenzi Mtendaji. http://community.co.tz/2013/03/20/ishara-za-mauaji-ya-kimbari-zi-wazi-tanzania-kijo-bisimba/
0 comments:
Speak up your mind
Tell us what you're thinking... !