CCM imeanza lini kuwa rafiki wa Waislamu? - Kitoloho
Headlines News :
Home » » CCM imeanza lini kuwa rafiki wa Waislamu?

CCM imeanza lini kuwa rafiki wa Waislamu?

Written By Msamaa on Saturday, May 11, 2013 | 1:53 AM



M. M. Mwanakijiji.
SOURCE:TANZANIA DAIMA{Jumatano,30 March 2011}
UTETEZI mkali wa Mufti Sheikh Shaaban Bin Simba kuitetea serikali ya CCM na hasa Rais Kikwete wiki iliyopita, umenifanya nibakie na swali moja ambalo bado sijapata jawabu lake la uhakika; ni lini Chama Cha Mapinduzi kimebadilika na kuwa rafiki ya Waislamu?

Ni swali la muhimu kwa sababu utetezi wake (na hata wa watu wengine) ulijikita katika suala la “sisi” dhidi ya “wao”. Ulikuwa ni utetezi unaosema kuwa “sisi” – Waislamu dhidi ya “wao” – wasio Wakristu. Kwa vile hoja hii ya udini inazidi kusukumizwa katika akili zetu hatuna budi kulizungumzia kwa sababu kuendelea kuikwepa ni kutoa kibali kuwa pande zenye mirengo ya kidini kuendelea kutulazimisha kukubaliana na hali iliyopo bila ya kuipinga.
Nina bahati ya kwamba nimekisoma kitabu kizima cha Profesa Hamza M. Njozi ambacho kilituelezea kwa kiasi historia ya mahusiano ya CCM na Waislamu nchini. Kitabu hicho ambacho kilipigwa marufuku nchini kinaitwa “Mauaji ya Mwembechai na Hatma ya Kisiasa ya Tanzania”.

Vile vile nimepata kusoma maandishi mengi ya mmoja wa wanaharakati wa Kiislamu nchini. Mohammed Said ambaye naye ameandika vitabu na insha kadha wa kadha ambazo ndani yame ametudokeza (wakati mwingine kwa kirefu) jinsi gani utawala wa CCM ulivyokuwa ukiwakandamiza Waislamu.
Dk. Njozi ambaye nilipata nafasi ya kufanya naye mahojiano ya kina miaka kama mitano iliyopita kuhusiana na kitabu chake hicho alinielewesha kwa kirefu sana jinsi gani utawala wa CCM haukuwa rafiki mzuri wa Waislamu.
Japo watu wengi wanafikiria kitabu cha Njozi kilipigwa marufuku kwa sababu ya madai yake juu ya mauaji ya Mwembechai binafsi baada ya kukisoma na kukielewa (hasa ambatisho la barua ya Abu Aziz kwenda kwa Mwanasheria Mkuu) nimegundua kuwa tatizo kubwa la kitabu hicho ilikuwa ni madai yake makali dhidi ya viongozi wa CCM na Chama Cha Mapinduzi.

Katika mjadala wa hivi karibuni na Said kwenye mtandao wa JamiiForums.com na baada ya kusoma maandishi yake mbalimbali ya huko nyuma niliweza kuelewa kwamba tatizo la Waislamu muda mrefu halikuwa dhidi ya Nyerere tu (hili la Nyerere ni la siku za karibuni zaidi) bali ulikuwa ni dhidi ya utawala wa CCM.
Kwa muda mrefu viongozi mbalimbali wa Kiislamu wamekuwa na matatizo na utawala wa CCM, sera zake, uongozi wake, ahadi zake na mipango yake. Kabla ya miaka hii miwili iliyopita viongozi wengi wa Waislamu walichukulia CCM kama ni sehemu ya tatizo linalotishia maslahi ya Waislamu.
Hata hivyo, inaonekana matatizo yote ambayo jamii ya Waislamu ilikuwa nayo katika miongo karibu mitano ya Uhuru wa Tanzania bara sasa yamekwisha. Madhambi na mambo yote ambayo tuliaminishwa kuwa ni matatizo ya Chama Cha Mapinduzi dhidi ya Waislamu yamesamehewa na kama maneno ya Mufti hivi karibuni ni ya kuaminiwa (na sioni sababu ya kutoyaamini) uhusiano mpya wa mapatano kati ya Chama cha Mapinduzi na Waislamu umeanza. Kuanzia sasa Jamii ya Waislamu imepoteza haki ya kuilalamikia CCM na serikali yake.

Jamii yetu hii imepoteza haki ya kulalamikia suala la Mahakama ya Kadhi kama ilivyopoteza haki ya kulalamikia suala la OIC. Mambo yote mawili yameliliwa na Waislamu kwa muda mrefu na baada ya kurushwa rushwa na kutokupewa majibu kamili yamebakia kama maneno matamu ya kuvutia. Sasa hivi wale wanaosimamia mambo hayo hawawezi tena kuyadai kwa nguvu bila kuonekana wako kinyume na serikali. Kilichobakia ni kutegemea wema na huruma ya CCM kuweza kupatiwa mambo haya.

Lakini haya yanavutia baadhi tu ya Waislamu na wala si Waislamu wote. Kitu ambacho kinanishangaza sana ni kujaribu kuangalia Waislamu kama watu wanaoongozwa na hitaji moja tu linalofanana. Sote tunafahamu kuwa hata kwenye nchi ambazo zina Waislamu wengi kama Saudia, Yemen, Oman, Libya, Misri, Syria, Iran, na hata Iraq Waislamu huunganishwa na maslahi mbalimbali zaidi ya yale ya imani.

Mtu yeyote ambaye alichukua muda kufuatilia au anayeendelea kufuatilia mwamko wa mabadiliko kwenye nchi hizo atagundua kuwa wananchi wa nchi hizo hawaandamani kwa sababu wanakandamizwa na tawala zenye kuongozwa na makanisa au ambazo tunaweza kusema kuwa zisizo za Kiislamu; la hasha viongozi wa nchi hizo zote ni Waislamu na baadhi ya nchi hizo zina mifumo ya Kiislamu ambayo inatawala.
Tungetarajia kwa mfano nchi kama Iran wananchi wake wote wangekuwa hawana malalamiko yoyote dhidi ya serikali ya Mapinduzi ya Kiislamu. Kwamba, kwa vile wanaongozwa kwa kiasi kikubwa na mifumo inayoendana na imani yao basi kusingekuwa na malalamiko ya kudai uhuru zaidi au demokrasia zaidi.

Hili ni kweli hata kwenye nchi kama Saudia ambako tungelazimika kuamini kuwa maslahi ya kila Muislamu yanalindwa. Lakini haikuwa hivyo; tunakumbuka kuwa baada ya wimbi la mabadiliko la Tunisia kupamba moto na pale mlipuko wa Uwanja wa Tahrir ulipozidi watawala wa Saudia kwa haraka wakatangaza kuongeza posho mbalimbali kwa wananchi wao!

Jawabu ambalo linaweza kutolewa mara moja ni kuwa nchi hizo zote ambazo ziko katika msuko suko wa kisiasa ziko karibu na Marekani na Israeli na hivyo wananchi wake ndio maana wameinuka dhidi yake. Hata hivyo, hilo halina ushahidi kwani yeyote ambaye amefuatilia matangazo ya Al-Jazeera ataona kuwa wananchi wa hizo wanachodai ni utu wao. Huwezi kuishi kwenye taifa ambalo kuna hali ya hatari kwa miaka thelathini na ukajiona kuwa uko huru! Huwezi kuishi kwa furaha katika nchi ambayo watawala wake wanashikilia nafasi zote za utajiri nawe ukajiona ni sehemu ya jamii hiyo?

Waislamu wa nchi hizo kumbe walitambua kile ambacho naamini ndugu zetu wa Tanzania walikitambua miaka michache iliyopita kwamba matatizo yao yanahusiana kabisa na utawala ulioko madarakani. Yeyote ambaye amewasoma vizuri kina Njozi na Said, Abu Aziz na waandishi wengine wa Kiislamu nchini ataona kuwa walielewa kile ambacho Wamisri na Wayemen wamechelewa kukielewa. Kile ambacho napendekeza kuwa Mufti Simba anataka Waislamu wakisahau mara kuwa matatizo yao yanahusiana na utawala ulioko madarakani - yaani utawala wa CCM.

Barua ya Abu Aziz iliyoko mwishoni mwa kitabu cha Njozi (Nyongeza ya 1) ina haya ya kusema juu ya CCM na Waislamu “the truth is that the CCM government has acted arbitrarily and is not alive to the grave situation into which it has plunged the country. By being biased and allowing itself to be duped by the Catholic clergy that Muslim preaching was insulting to Christianity, the CCM government has embarked on a course of action which violates the constitutional rights of Muslims to propagate religion, is arbitrary and without any regard to the due process of law.”

Yaani, “ukweli ni kwamba Serikali ya CCM imefanya kiholela na haionyeshi kujali dimbwi la hatari ambalo imeiingiza nchi. Kwa kuonesha upendeleo na kukubali kudanganywa na mapadri wa Kikatoliki kwamba mahubiri ya Waislamu yana kashfu Ukristu, Serikali ya CCM imejielekeza kuchukua hatua ambazo zinavunja haki za Kikatiba za Waislamu kutangaza dini, ni za kiholela na ambazo hazijali kabisa kufuata sheria” (Italiki na tafsiri zote toka Kiingereza zangu).

Hiyo ni sehemu ya hukumu kali ya Abu Zaid ambaye sehemu nyingine katika Waraka mrefu kwa Mwanasheria Mkuu akamka pasipo utata kuwa “The CCM government has used the criminal justice system to silence Muslims simply because they are exercising their constitutional right of propagating religion.
The response by the CCM government has been characterised by abuse of power.” Yaani, “Serikali ya CCM imetumia mfumo wetu wa sheria kunyamazisha Waislamu kwa sababu tu wanatumia haki yao ya Kikatiba kutangaza dini. Mwitikio huo wa CCM umeendana na matumizi mabaya ya madaraka”.

Naye Mohammed Said akiandika katika makala aliyoita “Islam and Politics in Tanzania” anapitisha hukumu hii dhidi ya CCM na Bakwata “The Party is weak, it no longer commands respect, dignity and enthusiasm it did in the days of yore. The Party has alienated itself from its founders. The de-Islamisation of the Party has gone full circle and its Muslim history has been erased. Bakwata has sided with the government thus failing to uphold Muslim values and principles.”

Kwamba, “Chama (CCM) ni dhaifu na hakina tena heshima, hadhi, na mvuto kilichokuwa nayo miaka ya nyuma. Chama kimejitenga na waasisi wake. Kuondolewa kwa kumbukumbu za Uislamu toka ndani ya chama kumekamilika na historia yake ya Waislamu imefutwa. BAKWATA imechukua upande wa serikali na hivyo kushindwa kusimamia tunu na kanuni za Kiislamu”.

Sasa haya yote ni ya kweli na ni madai mazito na kama nilivyodokeza hapo juu ndio sababu kubwa ya kitabu cha Njozi kupigwa marufuku nchini. Watu wengi wanafikiri kilipigwa marufuku kwa sababu ya kutuelezea na kutuwekea ushahidi wa yaliyotokea Mwembechai; la hasha. Nina uhakika hata Njozi akiulizwa leo atakubaliana nami kuwa sababu kubwa ni kuwa kitabu chake kiliweka bayana ile siri ambayo ilikuwa inajulikana pembeni kuwa CCM inahusika na matatizo ya Waislamu.

Sasa kama hili ni kweli - na bado sijapata sababu ya kuona kuwa siyo. Huu urafiki mpya ambao tumeuona hivi karibuni kati ya viongozi wa Kiislamu, makundi kadhaa ya Waislamu na Chama Cha Mapinduzi umetokana na nini? Ninajiuliza kuwa kauli ya Sheikh Mkuu Bin Simba kwamba “Misikiti iungurume na wala isikae kimya, ukimya ufe na yalaani mabaya yote hayo pamoja na dini ya Kiislamu kufanywa tabaka la chini, tuamke na tushikamane kwa pamoja.” Imetoka wapi?

Au kauli yake hii kwamba “Wanasiasa wanataka kuivuruga nchi kwa visingizio kuwa wanataka kulinda amani, hivyo Waislamu tumeamua kuvunja ukimya uliodumu kwa muda mrefu na kuamua kukemea vitendo hivyo” tunaweza kuipa uzito gani hasa ikizingatiwa kuwa amani ilipovunjwa mwaka 1998 na 2001 Bakwata hawakuwa wakali kwa serikali kiasi hiki?
Ni wazi kwamba BAKWATA nayo imeamua kujivika taji la kuitetea serikali ya CCM. Kwa Waislamu wengine hili si jambo geni (kama nilivyoonyesha hapo juu) kwani mara zote BAKWATA imekuwa ikisimama na serikali ya CCM.

Lakini pia kitu kipya ambacho kimetokea sasa hivi na hasa wakati wa kampeni ni kuwa hata wale viongozi wa dini ya Kiislamu ambao walikuwa kinyume na serikali ya CCM walijitokeza na wengi wanaendelea kujitokeza kuitetea CCM mbele ya umma. Sisi wengine tunajiuliza CCM ilibadilika lini na kuwa rafiki wa Waislamu?
Ninabakia na majibu kadha wa kadha kubwa ambalo laweza kuonekana ni kuwa hatimaye matatizo ya Waislamu yamepatiwa tiba ndani ya serikali ya CCM.

Kwamba sera na ahadi za CCM kuelekea 2015 ni bora zaidi kuliko wakati mwingine wowote na kuliko za chama kingine chochote. Kwamba uongozi wa CCM umeonyesha kuelewa matatizo ya Waislamu kuliko uongozi wa chama kingine chochote. Kama hii ni kweli; ina maana ya kwamba.

Ÿ Makosa yote ya CCM ambayo imeyafanya huko nyuma yamefutwa na kusamehewa rasmi na sasa Waislamu wote waiunge mkono CCM kwa sababu moja tu kuwa hatimaye maslahi yao kama Waislamu yamepata mtetezi;

Ÿ Madai yote ambayo yamekuwa yakitolewa dhidi ya Kanisa ambalo tuliaminishwa kuwa ndilo liko nyuma ya CCM - wengine walifikia kuiita CCM - Catholic Church Movement hayana ukweli tena - kwa sababu kama CCM bado ni Catholic Church Movement ina maana Waislamu wanaoiunga mkono CCM wanaunga mkono Kanisa Katoliki;

Ÿ Madai kuwa upo Mfumo Kristo hayana msingi wowote kwa sababu kwa miaka karibu hamsini Tanzania imekuwa chini ya Chama Cha Mapinduzi ambacho ndicho kilitengeneza mfumo wa utawala ambao leo unatetewa na kutafutiwa udhuru.

Hii ni kinyume na sisi wengine ambao tunaamini upo “MFUMO FISADI a.k.a MFUMO CCM” ambao umetunyang’anya haki zetu, kutudhulumu utu wetu na kutufanya tuwe kama wageni katika nchi yetu.
Ni mfumo ambao umeendeleza umaskini wa Waislamu, Wakristu na Wenye Imani za Jadi! Mfumo Kristo ni kisingizio, mfumo fisadi ni sababu!
Mfumo huu ambao leo unatetewa kwa nguvu zote unahitaji ujasiri mkubwa sana kutetewa.

Pamoja na hayo ni wazi tuamini kuwa yumkini kuna sababu nyingine kwani kwa kipimo chochote kile hakuna mabadiliko yoyote ambayo yametokea ndani ya CCM hata kuweza kudai kuwa CCM ni bora kwa Waislamu nchini; siyo tu kwa Waislamu lakini kwa Watanzania wote kwani maslahi ya Watanzania yote yanabeba ndani yake maslahi ya Waislamu, Wakristu, Wapagani na wasioamini kabisa!

Pendekezo ambalo limetolewa na Shehe Mkuu ambalo yumkini ndio msingi wa utetezi unaoendelea ni kuwa Rais Kikwete anatetewa kama Muislamu na si kwa sababu ya CCM. Kwamba, Waislamu wameamua kujitokeza kumtetea Muislamu mwenzao kwa sababu inaonekana Wakristu na Makanisa yanamshambulia na kushambulia utawala wake kwa sababu ya Uislamu wake. Kwa maoni ya watetezi wa misingi hiyo wanaona kuwa akija kiongozi Mkristu basi Wakristu watakuwa na haki ya kumtetea kwa misingi ya dini yake.
Kuhusu hili la “uenzetu huu” niliwahi kuandika Oktoba 12, 2009 katika makala yangu niliyoiita “Na Huu ‘Uenzetu huu’ tutashindwa kuwajibishana” nilisema hivi “Tutaanza kupiga hatua kubwa ya kuwakataa mafisadi pale tutakapoanza kukataa umoja nao na ushirika nao. Ukisikia fisadi ni Mkristu mwenzako, Muislamu mwenzako, Mnyakyusa mwenzako, Mhaya mwenzako; vuka hisia zako za “uenzetu” na umpime kwa matendo yake tu na umpinge vilivyo.

Ni lazima katika fikra zetu tuwe tayari kukataa dhulma, uonevu, wizi wa utajiri wetu, ubadhirifu, matumizi mabaya ya madaraka, ukandamizaji, unyanyasaji, unyonyaji wa aina yoyote ile na kwa mahali popote bila ya kujali unafanywa na nani au kama anayefanya tunafanana naye kwa namna yoyote. Vinginevyo, mafisadi hawa ambao ni wenzetu ndio kweli mafisadi wenzetu!”
Kwa sababu kama kuna Waislamu wanaomtetea Kikwete kwa sababu tu ya Uislamu wake (kama ambavyo Mufti anataka tuamini) basi ni wao ambao wanajiweka mahali pabaya sana;

Sera za CCM zinaweza kusababisha madhara mengi kwa watoto na familia za Waislamu lakini kwa sababu ni “mwenzetu” basi Waislamu wasilalamike;
Mipango ya maendeleo yaweza isisimamiwe vizuri lakini kwa vile ni “mwenzetu” Waislamu wasilalamike;
Shule za Kata ambazo zina changamoto nyingi zinaweza kuendelea kufanya vibaya na kuathiri watoto wengi wa Kiislamu lakini Waislamu wasipaze sauti kubwa kwa sababu ni “mwenzetu”;

Vitendo vya kifisadi kwenye taasisi za fedha na mikataba mibovu iliyogharimu mabilioni ya shilingi isilalamikiwe kwa nguvu zote hata kama fedha hizo zingeweza kutumika kuboresha mahospitali, mashule, kliniki, barabara, usafiri n.k visipigiwe kelele na Waislamu kwa sababu ya huu “uenzetu.”
Yote haya na mengine mengi yakikubaliwa ni tatizo zaidi. Kwa sababu, itakuwaje kama kiongozi ajaye wa Tanzania atakuwa ni Mkristu? Na itakuwaje kama atakuwa ni kiongozi toka nje ya CCM? Itakuwaje kama kuna chama nje ya CCM ambacho sera na mipango yake ni ya manufaa kwa Watanzania wote na si kikundi kimoja tu? Je, wale Waislamu wenye kuunga mkono CCM leo hii watakuwa tayari kukaa na CCM katika upinzani wakisubiri nafasi nyingine?
Hata hivyo hata baada ya kusema hayo yote bado kuna mambo mengi ya kutua moyo. Viongozi wa Waislamu hawawazungumzii Waislamu wote kwani Waislamu siyo kundi moja linalofanana kwa kila kitu (homogenous).

Waislamu wa Tanzania kama walivyo Watanzania wengine wana maslahi zaidi ya kukubaliana kidini. Wakiumwa wanaenda kwenye mahospitali yale yale wanayoenda Wakristu na Wenye imani za jadi; wakisafiri wanapita barabara zile zile; shule wanazosoma za umma ni zile zile wanazosoma watu wengine; polisi wanaowalinda ni wale wale wanaowalinda Watanzania wengine n.k
Kumbe kuna kundi la Waislamu ambalo halijanunuliwa na “huu uenzetu huu”. Kundi hili ni la vijana na wazee ambao wanatambua kuwa maslahi yao hayana tofauti na maslahi ya Watanzania wengine. Kundi hili linataka elimu bora kama wanavyotaka Watanzania wengine; wanataka mafao bora ya uzeeni kama wanavyotaka Watanzania wengine; wanataka mishahara mizuri kama wanavyotaka Watanzania wengine na wanataka maisha bora yenye hadhi na utu wa mwanadamu kama wanavyotaka Watanzania wengine. Kundi hili la Waislamu halikubali ghilba ya kidini kwani linajua wazi kuwa kufanikiwa kwa Tanzania nzima ni kufanikiwa kwa kila Mtanzania.

Hili kundi limesoma, halishawishiwi kwa maneno ya kidini tu au ya kiimani lakini linajuliza maswali ya msingi na linatafuta majibu ya kweli. Kundi hili linauwezo wa kuchambua mambo kwa kusababisha maswali ya msingi yajibiwe kwanza kabla halijarukia kwingine.
Linajiuliza kwa mfano kwanini leo tuambiewe tuiunge mkono CCM wakati miezi michache tu CCM ilikuwa ndio adui yetu? Kwanini tumtetee Kikwete kwa sababu ya dini yake tu lakini tusihoji uongozi wake? Je ni kweli mfumo Kristo upo au upo Mfumo Fisadi ambao unaathiri Waislamu kama unavyoathiri Wakritu na Wapagani? Je, tunaweza kufanikiwa kama Waislamu tu bila kuhakikisha tunafanikiwa kama Watanzania?

Kundi hili ndilo ambalo unaliona likijitenga na siasa za kidini na kuunga mkono upinzani wa kweli na haliogopi kujitokeza kufanya hivyo. Kundi hili halijalishi wachungaji au mapadre wanasema nini kwani linajua kinachotaka.
Kundi hili haliogopi kushirikiana na Watanzania wengine katika kuupinga mfumo dhalimu wa kifisadi kwa sababu ni katika kufanya hivyo linajitengenezea lenyewe, na Watanzania wengine mazingira ambapo kila Mtanzania atapata nafasi nzuri ya kufanikiwa na kuishi kwa uhuru, amani na utu bila kujali rangi, dini, kabila, mahali, hadhi au nafasi.
Ninaamini kabisa kuwa kundi hili ni kubwa lakini lililo kimya (the silent majority) na ambalo linatambua bila ya shaka kuwa tatizo la Tanzania linahusiana kabisa na CCM.
Hili ni kundi ambalo linahofiwa sana na watawala kwa sababu likijitokeza wazi na kuunga mkono harakati za mabadiliko ya kweli (na nina uhakika litafanya hivyo siku si nyingi) ambayo yatamnufaisha kila Mtanzania - CCM itakuwa imepoteza karata ya mwisho ya kuishikilia Tanzania kama paka anavyobeba kitoto chake shingoni, yaani Udini.
Share this article :

0 comments:

Speak up your mind

Tell us what you're thinking... !

ZILIZOSOMWA SANA.

Followers

Blog Archive

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Proudly powered by Blogger
Copyright © 2011. Kitoloho - All Rights Reserved
Template Design by Creating Website Published by Mas Template