Kila la kheri Zanzibar, bye bye Muungano! - Kitoloho
Headlines News :
Home » » Kila la kheri Zanzibar, bye bye Muungano!

Kila la kheri Zanzibar, bye bye Muungano!

Written By Msamaa on Saturday, May 25, 2013 | 12:43 PM

Makala
Hoja yangu
 
Lula wa Ndali Mwananzela
CHANZO: RAIA MWEMA.
Toleo la 250
18 Jul 2012
TUMEFIKA mahali na wakati ambapo yatupasa tuliseme lililo dhahiri; kila la kheri Zanzibar, bye bye Muungano! Hakuna sababu ya kupigania Muungano usiokuwapo; na Muungano usiokuwapo ambao pia ni dhaifu kupita kiasi haufai kutetewa hasa kama hauna watetezi. Baada ya kusema kauli zilizonukuliwa za mjane wa mzee Abeid Karume nahitimisha pasi na shaka kuwa, mwamko wa kudai kuvunjwa kwa Muungano ambao unaendelea Zanzibar si wa kikundi cha kidini kama tunavyotaka kuaminishwa bali ni mpango uliobuniwa madhubuti na wanasiasa wa Zanzibar ambao hawataki kuendelea kuwapo kwa Muungano.

Nikitambua ukweli wa sauti tunazozisikia kutoka Zanzibar na hasa kukosekana kwa sauti thabiti zenye kutetea Mapinduzi ya Zanzibar ambayo yalizaa Muungano sina shaka yoyote kuwa hakuna namna nyingine yoyote ya kuuokoa Muungano,. isipokuwa kuuvunja kwanza ili kila mtu aende na zake. Kama imefika mahali hata mama Karume – ambaye mumewe na mwanae wamewahi kuwa marais Zanzibar anaona kuwa hakuna faida ya Muungano na anakubaliana na madai ya wanauamsho wa Zanzibar hakuna namna nyingine isipokuwa kuharakisha kujitoa kwa Zanzibar kwenye Muungano ili waende na kuwa kile kisiwa cha neema ambacho kiliahidiwa na wazee wako tangu enzi na enzi!

Mazingira yaliyoibua Muungano hayapo tena
Mazingira yaliyosababisha Muungano mwaka 1964 hayapo tena. Wakati Muungano unatokea wakati ule Afrika ilikuwa katika harakati za uhuru na nchi nyingi za kiafrika zilikuwa zinatoka kwenye makucha ya wakoloni huku nyingine – kama Namibia, Zimbabwe na Msumbiji (nikizitaja chache) – zikiwa kwenye harakati za uhuru.

Mazingira hayo ya kisiasa hayakuwa yameishia katika harakati za uhuru tu bali pia mgawanyiko wa kambi mbili za dunia katika Vita Baridi ulikuwa umekamilika. Miaka miwili nyuma dunia ilikuwa katikati ya hatihati ya kuingia katika vita vya kinyuklia kutokana na mgogoro wa silaha wa Cuba. Hofu iliyotokea baada ya Mapinduzi ya Zanzibar ni hisia kuwa Zanzibar ingeweza kugeuka kuwa “Cuba ya Africa”.

Hata hivyo, mazingira makubwa zaidi ya kuondolewa kwa usultani uliodumu kwa karne karibu tatu yalikuwa ni tishio kubwa kwa watawala wapya wa Zanzibar. Hakuna mtu aliyetarajia kuwa usultani ungeweza kuondolewa katika saa chache na watu wenye silaha duni. Tishio la jaribio la kumrudisha sultani kwa wakati ule lilikuwa dhahiri. Kwa watu wanaokumbuka historia Sultan Jamsheed aliomba msaada wa askari kutoka Tanganyika kuzima mapinduzi kitu ambacho Nyerere hakukubali.
Sultani hakupata msaada wowote kutoka bara na msaada wa kutoka kwa binamu zake wa Oman usingeweza kuelekea visiwani hapo bila kusababisha watu wa bara kuingilia kati na hata mataifa ya Magharibi yaliyokuwa na maslahi visiwani humo yasingekaa pembeni.

Ili kuiokoa Zanzibar Tanganyika ilijitoa muhanga kwa kila namna hadi kukubali kufa ili Zanzibar iwepo. Narudia sentensi hii, ili Wazanzibar wajue kuwa Tanganyika haijawahi kuwa adui wa Zanzibar bali imekuwa ni zaidi ya rafiki; imekuwa ni ndugu. Tanganyika haikuwa ndugu wa maneno; ilikuwa ni ndugu aliyekuwa tayari kufa ili mdogo wake aishi. Tanganyika imekufa ili Zanzibar iwepo.
Leo Zanzibar imekomaa na kunusurika na tishio kubwa ndani yake Tanganyika inaambiwa ni mkoloni. Tatizo ni kuwa Tanganyika kwa kweli haikufa kabisa; ilikubali kulazwa nusu kaputi ili kuokoa uhai wa Zanzibar. Sasa Tanganyika inaamka!

Tanganyika ilikubali kuua uhuru wake ili Zanzibar iwe huru nayo. Kujitoa huku muhanga kwa Tanganyika kwa wanaofahamu historia hakukuwa kwa maneno matupu tu. Wengi – wanaofahamu historia- wanakumbuka kuwa Nyerere alikuwa tayari hata kuahirisha uhuru wa Tanganyika ili lipatikane shirikisho la Afrika Mashariki chini ya Mzee Jomo Kenyatta. Na kujitoa huku muhanga kuliendelea katika harakati za ukombozi kusini mwa Bara la Afrika. Lakini hakuna mahali ambapo Tanganyika ilijitoa mhanga zaidi kama ilipokuja suala la Zanzibar. Ili kuiokoa Zanzibar, Tanganyika iliacha Zanzibar ibakie na serikali yake, uongozi wake, chama chake na hata mwelekeo wake.
Kinyume na inavyolalamikiwa na wengi jitihada za kuirejesha Zanzibar katika uhai wake zilianza miaka karibu 30 nyuma. Zanzibar ikapata baraza lake la kutunga sheria, Zanzibar ikapata katiba yake, Zanzibar ikapata wimbo wake wa taifa, na bendera yake na Rais wake mtendaji na hivi karibuni Zanzibar ikajitaja kuwa ni nchi kamili.

Wakati huu wote Tanganyika imeendelea kuilea Zanzibar ili ipate uhai wake; tulidhania – kwa makosa makubwa – kuwa Zanzibar itatambua kuwa ina undugu na ukaribu na Tanganyika kiasi cha kutaka hatimaye kuwa nchi moja kamili. Walipopata vyote Zanzibar wanasema wanataka kutoka. Sasa ni jukumu la Tanganyika kuwasaidia kutoka.

Tumechoka kunyonywa!
Zanzibar imekuwa kama kupe mgongoni mwa ng’ombe. Haiishi kulalamika kwa nini ng’ombe hali vizuri, kwa nini ng’ombe hatambui uwepo wa kupe, kwa nini ng’ombe damu yake si tamu sana.
Imekuwa ni kupe asiyetosheka na sasa anaamini kuwa kwa kujitoa mgongoni mwa ng’ombe anamkomoa ng’ombe. Ati anadai uhuru wake, ili awe kupe kamili. Tatizo ni kuwa hakuna namna yoyote kupe ataweza kukaa bila kunyonya ng’ombe au mnyama mwingine. Zanzibar haiwezi kukaa bila kutegemea nchi nyingine. Ama itategemea bara au itajaribu kutegemea Uarabuni au nchi nyingine.

Haina uwezo wa kusimama yenyewe hata watu wake watamanie vipi. Tumaini pekee kuwa ikipata mafuta itageuka pepo ni ndoto za Alinacha. Hata yakipatikana mafuta kesho inachukua miaka mingi kuweza kubadilisha maisha ya wananchi. Ila yakipatikana mafuta Zanzibar kizazi cha watawala kitanufaika sana hilo halina shaka. Ndio kanuni ya “laana nyeusi”. Nani anatawala Zanzibar?
Sasa sisi wa bara nao tumekuwa wavumilivu mno na uvumilivu wa kutukanwa, kukejeliwa na kudharauliwa na ‘kanchi’ kama Zanzibar umetuisha. Kwa nini leo sisi tuliotoa “so much” kwa ajili ya Zanzibar kuonekana leo ati ndio “wakoloni”?

Leo hii tunatajwa kwa kejeli, muasisi wa taifa letu akitukanwa hadharani na mtu pekee ambaye aliiokoa Zanzibar na kuipa uhai wake aonekane ni kituko? Wakati wa kusema “imetosha” umefika. Zanzibar iamue kuondoka, na iondoke mwaka huu! Hakuna haja ya kura ya maoni – wamuulize nani kama hadi mke wa Karume anaposimama na kubeza Muungano? Wamuulize nani wakati leo kitu ambacho kisingiwezekana Zanzibar (Mpemba kutawala visiwa hivyo) kinawezekana kwa sababu ya Muungano na hakuna mwenye ujasiri wa kujibu hoja dhidi ya Muungano?

Zanzibar inapewa upendeleo ambao hakuna eneo jingine lolote la Muungano linapewa. Inapewa upendeleo katika elimu, jeshi, ubalozi na hata fedha. Ni wananchi wa mkoa gani wa Tanzania ambao wanaweza kudai vinavyodaiwa na Zanzibar? Tumesikia watu wa Mtwara wakidai upendeleo wa pekee kwa sababu na wao ni sehemu ya Muungano? Tumesikia lini wananchi wa Singida wakisema nao wao wapewe ubalozi, au uwakilishi kwenye taasisi mbalimbali kwa kuangalia asilimia ya makabila mengine (hasa Wanyakyusa, Wahaya, na Wachagga)? Hakuna; lakini Zanzibar wanaweza kusimama na kudai upendeleo huu ati kwa sababu “zilizoungana ni nchi mbili”! Wakati huo huo hakuna mbara hata mmoja ambaye amewahi kusimama kudai kuwa Serikali ya Zanzibar itoe nafasi kwa wabara ili kuimarisha Muungano!

Lini umesikia muswada umepitishwa Zanzibar kutoa upendeleo kwa wananchi wa Mafia? Au wananchi wa Kilwa? Hawawezi kwa sababu mara moja watadai “udogo wa visiwa”!
Sasa cha Tanzania ni cha Watanzania wote (wakiwemo Wazanzibari) lakini cha Zanzibar ni cha Wazanzibari wote na si cha Mtanzania yeyote. Kwa nini tuendelee na mfumo huu wa kinyonyaji? Kwa nini tuendelee kuipa Zanzibar upendeleo usiostahili. Zanzibar ina wasomi wengi na ina watu wengi wako nje na wengi wako Bara; wakati umefika hawa wote warudi Zanzibar na kuanza kujenga nchi yao. Waachilie nafasi zao kwenye Muungano – kwa kuanzia na Dk. Ghaib Bilal na wengine wote ili nafasi hizo zishikwe na Watanganyika.

Tuwasaidie Wazanzibari waache maandamano
Sasa sisi watu wa Tanganyika (Tanzania proper) tunaweza kuwasaidia Wazanzibar kuondoka kwenye Muungano ili waweze kujenga taifa lao jipya lenye maziwa na asali; taifa ambalo wakipiga zumari hadi maziwa makuu wanacheza; taifa ambalo kila mtu anaishi kwa furaha na kula halua na tende huku wakicheza gombe sugu! Tuwasaidie Wazanzibar watoke kwenye Muungano mapema zaidi kuliko ilivyo sasa.

Tusiwaache wafanye makongamano na maandamano yasiyoisha kudai “uhuru kamili” wakati njia ya kuwapatia uhuru “kamili” ni rahisi sana. Niliandika huko nyuma kuwa njia rahisi zaidi ya kuwaondoa Zanzibar kwenye Muungano ni kuwahamiza wawakilishi wao – kina Jussa na wenzake – waandike sheria ya kura ya maoni ya kutoka kwenye Muungano na waitishe kura yao kabla ya mwisho wa mwaka huu ili hatimaye ifikapo Disemba 31, 2012 Zanzibar iwe taifa huru nje ya Muungano. Miezi imepita na sioni juhudi zozote za Wazanzibari kutoka kwenye Muungano zaidi ya kuendelea kutuambia kuwa wanataka kutoka!

Sasa kwa vile kina Jussa hawana ujasiri huo na kwa vile wana uamsho hawana uwezo wala ujasiri wa kuwashawishi wawakilishi wao kuitisha kura ya maoni mapema ili watoke kwenye Muungano sisi upande wa Tanganyika inabidi tuwasaidie. Siyo kwa kuidai Tanganyika kama wengine wanavyotaka tufanye; la hasha. Tukiidai Tanganyika maana yake tunataka Zanzibar iwepo na Tanganyika iwepo ili kuwe na serikali tatu. Sasa tukiwa na serikali tatu bado Tanganyika italipa gharama kubwa zaidi ya kuiendesha.

Kwa sababu huwezi kuwa na serikali tatu ambazo hizo serikali mbili zinachangia 50 kwa 50, kwa sababu mara moja itaonekana Zanzibar inanyonywa. Itakuwaje watu milioni 45 wachangie sawa sawa na watu milioni mbili? Wazanzibari hawa hawa wataanza kulia kuwa Tanganyika inawanyonya bado na watataka tuchangie kwa “asilimia” huku wao wakitaka kuchangia asilimia kidogo kwa sababu ni ‘wachache’ na uchumi wake ni ‘mdogo’. Tusikubali mkenge wa kudai Tanganyika.

Njia pekee ya kuwasaidia Wazanzibari kutoka kwenye Muungano ili wasitusababishie maumivu ya kichwa ya kudumu ni kudai Tanzania moja, nchi moja. Kwa vile Rais Kikwete na CCM wanasema hawataki tuuvunje Muungano bali tujadili “muundo wa Muungano” naomba nipendekeze kuwa muundo pekee unaofaa kwa Muungano ni wa “nchi moja, taifa moja”.
Hakuna mantiki ya kuwa na “nchi mbili ndani Muungano”. Haiingii akilini uwe na “nchi ndani ya nchi”. Sasa kama nchi iko ndani ya nchi haiwezekani kuwa na nchi mbili; bali moja. Ukiunganisha maji na maji, huwi na maji mawili bali maji tu!

Sasa njia pekee ya kuwasaidia kuondoka kwenye Muungano ni kudai “nchi moja taifa moja”. Inapopita timu ya kukusanya maoni ya Katiba Mpya na linapokuja suala la Muundo wa Muungano watu wa bara wasidai “serikali tatu”. Wadai “serikali moja”. Yaani kutakuwa na serikali ya Muungano na tawala za mahali au serikali za mahali na mahali. Tayari tumeshakuwa na serikali mbili na zimetuletea matatizo haiwezekani tukafikiria kuwa tukiongeza serikali ya tatu tutakuwa tumepunguza matatizo. Haiwezekani ukiwa na mtoto mmoja uone ni tatizo halafu ukiwa na watatu utakuwa umepunguza!

Hivyo, watu wa bara tunajua kabisa tukiimeza Zanzibar rasmi – hakuna cha BlW (Baraza la Wawakilishi), hakuna Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, hakuna bendera wala wimbo wa “taifa” la Zanzibar na hakuna Rais wa Zanzibar wala chochote cha ‘Zanzibar”. Tunapoamua kuimeza ndani ya taifa moja Zanzibar inakuwa sehemu kweli ya Jamhuri ya Muungano. Hili pendekezo ndilo ambalo watu wa bara tunahitaji kulisimamia na kulidai kwenye mchakato huu wa Katiba Mpya.
Kwa sababu Wazanzibar wenye uchungu na nchi yao hawawezi kukubali. Hawawezi kukubali Zanzibar imezwe kabisa. Watakataa na wataamua bora watoke. Uchaguzi utakuwa ni kumezwa au kutoka na wao watachagua kutoka – kitu ambacho ndicho tunataka kuwasaidia kufanya. Sasa wakishatoka Zanzibar isifikirie itakuwa na upendeleo maalumu kwa Tanganyika.

Baadhi ya vitu vya kwanza ambayo serikali ya Tanzania Mpya itahitaji kufanya ni kuweka masharti makali ya ukaazi na uzawa ili kwamba Wazanzibar wasije wakajipitisha kama Watanganyika. Pamoja na hilo kuweka usimamizi mzuri wa kodi ili kuhakikisha vitu vinavyoingia kutoka Zanzibar vinakidhi kiwango cha bara na kodi nyingine muhimu. Tusije tukaacha kuwa baada ya kutoka Wazanzibari wakaanza kupata upendeleo ambao walikuwa bado wanaupata. Tutatumia vigezo vile vile vya kuhusiana na nchi kama Wakenya, Waganda na Wanyarwanda.

Ndugu zangu katika kuendeleza kampeni hii ya Let Zanzibar Go ambayo tumeiasisi tuanze kuitakia kila la kheri Zanzibar na kusema “bye bye” Muungano. Tuwasaidie watoke kwenye Muungano kwa kuanza kutaka kuundwa kwa serikali moja – na si tatu. Hii ndio njia pekee, ya uhakika ya kuweza kuzungumzia suala la “muundo wa Muungano” bila kutaka kuuvunja moja kwa moja (kitu ambacho sheria ya katiba inakataza). Tukiidai serikali moja Wazanzibar hawatotaka watatoka nasi tutaipata Tanganyika yetu na ili kuzidi kuwaudhi maadui wa Muungano bado itapewa jina la Tanzania; au tukipenda kurudisha jina la kale zaidi la AZANIA!

Share this article :

0 comments:

Speak up your mind

Tell us what you're thinking... !

ZILIZOSOMWA SANA.

Followers

Blog Archive

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Proudly powered by Blogger
Copyright © 2011. Kitoloho - All Rights Reserved
Template Design by Creating Website Published by Mas Template