- Kitoloho
Headlines News :
Home » »

Written By Msamaa on Tuesday, May 7, 2013 | 11:16 AM

Waarabu wanne mbaroni
• Pinda aenda Arusha, viongozi wa dini wataka utulivu

na Mwandishi wetu
RAIA nane wakiwemo wanne wenye asili ya Kiarabu kutoka nchini Saudi Arabia na Watanzania wanne wanashikiliwa na Jeshi la Polisi mkoani Arusha kwa tuhuma za kuhusika na mlipuko wa bomu lililotokea katika uzinduzi wa Kanisa la Mtakatifu Joseph, Parokia ya Olasiti mkoani Arusha, juzi.
Habari ambazo Tanzania Daima imezipata kutoka jeshi la polisi mkoani Arusha, zinadai kati ya Watanznaia wanaoshikiliwa mmoja anatoka Babati ambaye ndiye anayedhaniwa kurusha bomu hilo.
Kwa mujibu wa chanzo kimoja cha habari, raia hao wa Saudi Arabia walikamatwa juzi mchana wakiwa njiani kuelekea Namanga mpakani mwa Tanzania na Kenya.
Inadhaniwa watu hao walikuwa wakitoroka hapa nchini, lakini walishindwa kufikia azma yao hiyo kutokana na msako mkali wa Jeshi la Polisi ulioanzishwa baada ya kutokea kwa tukio hilo.
Kwa mujibu wa chanzo hicho, watuhumiwa hao walihojiwa jana mchana katika ofisi za makao makuu ya polisi mkoani Arusha ambapo hata hivyo Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabasi, hakuwa tayari kueleza kile walichokisema.
Wakati huohuo Waziri Mkuu, Mizengo Pinda jana alikwenda mkoani Arusha katika eneo la tukio akazungumza waumini kanisani na baadaye kwenda kwa balozi wa Vatikan hapa nchini na mwakilishi wa Papa Francis, Askofu Fransisco Padilla.
Waziri Mkuu leo anatarajia kwenda katika Hospitali za KCMC na Mount Meru kuwajulia hali wagonjwa waliojeruhiwa na mlipuko huo ulioutikisa mji wa Arusha.
Wakati huohuo viongozi wa dini, serikali na vyama vya siasa nchini wameungana kutaka utulivu na uvumilivu katika kipindi hiki ambacho taifa limo katika hali ya sintofahamu kutokana na tukio la kigaidi la kushambuliwa waumini wa Kanisa Katoliki, mjini Arusha, juzi.
Waumini hao walifikwa na mkasa huo juzi majira ya saa 4 asubuhi wakiwa katika Misa ya Jubilee ya miaka 50 ya Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Arusha.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti, Rais wa Baraza la Maakofu Tanzania (TEC) Mhashamu askofu Tarcisius Ngalalekumtwa na Sheikh wa BAKWATA wa mkoa wa Dar es Salaam, Alhad Mussa Salim, wamewataka Wakristo na Waislam kuwa watulivu na kuviacha vyombo vya usalama vifanye kazi ya kuchunguza wahusika wa tukio hilo.
Wakati viongozi wa dini nchini wakionyesha mshikamano huo, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete jana alikatiza ziara yake ya kiserikali nchini Kuwait na kurejea nyumbani kuungana na viongozi wenzake wa serikali na dini kushughulikia tukio hilo.
Akitoa taarifa ya Rais Kikwete kukatiza ziara yake, Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu, Salva Rweyemamu, alisema kuwa Rais Kikwete alitarajiwa kurejea nyumbani leo, lakini alilazimika kukatiza ziara hiyo na kurejea nyumbani mara moja kuwa karibu na wafiwa pamoja na wale waliojeruhiwa katika shambulio hilo la kigaidi.
Akizungumza katika mahojiano maalumu na gazeti hili ofisini kwake mjini Iringa, Askofu Ngalalekumtwa, alisema kwamba ni utamaduni wa Wakristo wote duniani kuzidisha sala na maombi wakati wanaposhambuliwa na kudhuriwa ili atoe jibu kwa wanaohusika na vitendo hivyo.
“Kasi ya sala iendelee ili Mungu wetu wa Amani ajenge fikira za upendo na haki katika mioyo yetu, sala ndiyo silaha yetu pekee na tunaamini Mungu atatujibu kwa kuwafichua watu waliohusika na vitendo hivi vya kihalifu,” alisema askofu Ngalalekumtwa.
Aliwataka waumini kuwa watulivu na kutokata tamaa kuomba kwani Mungu ndiye mwenye jibu na atatoa majibu kadiri atakavyo kwa wale wote wanaowatesa wenzao kwa sababu zao binafsi.
“Tulieni na kufanya tafakuri kisha mwambieni Mungu hayo yote ayafanyie kazi kwa uweza wake. Sisi binadamu tunategemea nguvu kutoka kwake,” alisema na kuongeza: “Waliopoteza maisha wapokee Rehema ya Mungu na waliojeruhiwa wafarijiwe na uwezo wa Mungu,” alisema.
Alisema kuwa wakati huu ni wa kutafakari na kumkabidhi Mungu yale yote yanayowasumbua wanadamu na kuongeza nguvu ya sala ili majibu ya Mungu yapatikane kwao.
Kwa upande wake Sheikh wa mkoa wa Dar es Salaam Alhad Mussa Salim amewataka Watanzania kuwa watulivu na wavumilivu na kujizuia kutuhumiana au kutoa matamshi yenye kuchochea mgawanyiko wa kidini baina yao, wakati huu vyombo vya usalama vinapoendelea na uchunguzi wa tukio hilo la kigaidi.
“Kwanza kabisa nawapa pole waliofiwa na ndugu zao katika shambulizi hilo, na ninawatakia kheri ya kupona haraka wale wote waliojeruhiwa. Pili ninawaomba Watanzania kuwa watulivu na wavumilivu wakati huu vyombo vya usalama vinapofanya uchunguzi wa wahusika wa shambulizi hilo, tusianze kunyosheana vidole na kutoleana kauli za kufarakana kidini,” alisema Salim.
Naye mwenyekiti wa taasisi ya Imam Bukhary ya jijini Dar es Salaam, Sheikh Khalifa Khamis, ameitaka serikali kuyadhibiti haraka makundi ya Waislam yanayoeneza chuki na kuhamasisha kuua watu, kuchoma nyumba za ibada za dini zingine ili kulinda na kudumisha utulivu na amani ya nchi.
Alitaka viongozi wa dini, hasa wa Kiislam kutokubali dini yao kutumika na vikundi hivyo kama anuani ya kufanya maovu na kwamba wapaze sauti na kukana maovu hayo kwamba hayahusiani na imani ya Kiislam.
Alisema kuwa ni wakati muafaka sasa kwa masheikh kutumia njia zinazowezekana ili kuwafahamisha Waislam katika misikiti yao, mikutano mbalimbali ya hadhara na katika shughuli za kidini kwamba ni lazima kufuata mfumo wa Uislam unaokataza maovu.
Alisisitiza kuwa mafundisho ya dini, yanasisitiza amani, upendo baina ya watu wote, na ndio utamaduni ulioenziwa tangu zamani, hivyo si sahihi kutumia mgongo wa dini kufanya mambo yanayokwenda kinyume na sheria.
Sheikh Khalifa alinaani kitendo cha mauaji ya watu wasiokuwa na hatia yaliyofanywa na magaidi mjini Arusha na kuongeza kuwa vitendo hivyo ni ukiukwaji wa haki za binadamu.
Aidha kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Freeman Mbowe ametuma salaam za pole na rambirambi kwa waumini wa Kanisa Katoliki nchini na Watanzania wote kwa ujumla kutokana na shambulizi hilo lililotokea katika Kanisa la Olasiti, jijini Arusha, lililosababisha vifo na majeruhi, huku wengine wakipatwa na mshtuko mkubwa kutokana na tukio hilo.
Kwa mujibu wa taarifa ya ofisa habari wa CHADEMA, Tumaini Makene, kwa vyombo vya habari, Mbowe alitoa salaam hizo alipozungumza kwa njia ya simu na Katibu wa Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC), Padri Antony Makundi, juzi Jumapili jioni, baada ya kupata taarifa za tukio hilo la kigaidi.
Mbowe, ambaye pia ni Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni (KUB) aliwataka Watanzania wote kuwa watulivu wakati huu, ambapo serikali kupitia vyombo vya dola inafanya uchunguzi wa tukio hilo.
Aliitaka serikali kuchunguza na kutoa taarifa haraka kuhusu tukio hilo na matukio mengine yote ya namna hiyo ili kuwapatia Watanzania matumaini ya kuendelea kuishi kwa utulivu na amani katika nchi yao.
Baadhi ya wakazi wa kawaida wa jiji la Dar es Salaam wamelitupia lawama Jeshi la Polisi nchini kuwa ndio chanzo cha mashambulizi ya Arusha kutokana kushindwa kuwakamata baadhi ya watu tangu kuibuka kwa vitenodo hivyo.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti na Tanzania Daima jijni Dar es Salaam jana, kuhusu tukio la kushambuliwa watu waliokuwa kanisani juzi, wakazi hao walisema kama jeshi hilo halitakuwa makini huenda vitendo hivyo vikazidi kuendelea nchini.
Walisema kuna matukio ya kushambuliwa viongozi wa kidini, mgogoro kuhusu kuchinja na kutekwa na kuteswa kwa baadhi ya watu kutokana na mazingira ya kazi zao hata hivyo, hadi leo hakuna aliyekwishakamatwa kuhusiana na matukio hayo.
Mmoja wa wakazi hao Mushi Shayo, alisema huu si wakati wa kunyoosheana vidole bali wanaopaswa kulaumiwa ni jeshi la polisi kutokana na kushindwa kwao kuwabaini watu hao wanaoleta chokochoko za kigaidi.
Alisema kutowataja watu waliohusika na matukio mbalimbali ndiko kunakochangia baadhi ya watu hao wabaya kuendelea kufanya vitendo vyao hivyo.
Naye mwanaharakati, Amos Joseph, alisema umefika wakati kwa Watanzania kuacha kushabikia mambo bila kujua matokeo yake kwani wataipeleka nchi pabaya.
Alisema kuna watu hivi sasa wamekwishayapa muelekeo mashambulizi hayo kuwa yalifanywa na watu wa upande fulani kitendo ambacho kinazidi kujenga uhusiano mbaya katika jamii.
Tayari jeshi la polisi nchini limesema kuwa linawashikilia watu wanane kwa tuhuma za kuhusika na mlipuko huo, wanne kati yao ni raia wa Saudi Arabia na wengine ni Watanzania.
Mlipuko huo ulitokea katika kanisa Katoliki la Mtakatifu Joseph Parokia ya Olasiti Arusha mjini, juzi Jumapili, na kusababisha vifo vya watu wawili na kujeruhi 70.
 
SOURCE:TANZANIA DAIMA.
Share this article :

0 comments:

Speak up your mind

Tell us what you're thinking... !

ZILIZOSOMWA SANA.

Followers

Blog Archive

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Proudly powered by Blogger
Copyright © 2011. Kitoloho - All Rights Reserved
Template Design by Creating Website Published by Mas Template