- Kitoloho
Headlines News :
Home » »

Written By Msamaa on Friday, May 10, 2013 | 12:43 PM

Ponda huru
*Aachiwa kwa masharti ya kulinda amani
*Atakiwa awe na tabia njema kwa miezi 12
*Asindikizwa na polisi hadi nyumbani

Sheikh Ponda Issa Ponda
SAUTI za "Takbir ... Takbir ..." zilitawala katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jana baada ya Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania, Sheikh Ponda Issa Ponda na wenzake 49 kuachiwa huru katika kesi iliyokuwa ikiwakabili. Washtakiwa hao waliachiwa huru na Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Victoria Nongwa.

Katika kesi hiyo upande wa Jamhuri uliwakilishwa na Wakili wa Serikali Mwandamizi, Tumaini Kweka na upande wa utetezi uliwakilishwa na Wakili Yahya Njama.

Akisoma hukumu Hakimu Nongwa alisema: “Jamhuri imeshindwa kuthibitisha mashtaka kuanzia shtaka la kwanza, tatu, nne na la tano kwa washtakiwa wote, katika mashtaka hayo washtakiwa wote kuanzia wa kwanza hadi 50 hawana hatia.

“Katika shtaka la pili la kuingia kwa nguvu katika uwanja wa Markaz Chang’ombe, upande wa mashtaka umeweza kuthibitisha kwamba Ponda aliingia kwa nguvu hivyo anatiwa hatiani kwa kosa hilo.

“Shtaka la kuingia kwa nguvu halielezi adhabu inayostahili kutolewa lakini mahakama inaweza kumpa adhabu ya kifungo cha miaka miwili jela au faini au vyote kwa pamoja.

“Kwa mshtakiwa wa kwanza (Ponda) hakuna kumbukumbu kwamba ni mkosaji wa makosa mengine… mahakama inazingatia pia mshtakiwa alikaa rumande kwa muda mrefu kuanzia Oktoba 18 mwaka jana hadi leo hivyo inamwachiwa kwa masharti.

Alisema mahakama inamwachia Ponda kwa masharti ya kulinda amani, awe mwenye tabia njema kwa miezi 12 na endapo atashindwa atarudi mahakamani apewe adhabu nyingine inayostahili.

Ponda alisaini fomu za kukubali masharti aliyopewa na kuachiwa huru huku wafuasi waliorundikana nje ya mahakama wakimsubiri kwa ajili ya kumlaki.

Hata hivyo ndoto zao zilizimwa na polisi ambao waliamuru asitoke nje kwa miguu.

“Hakuna usitoke nje…. Gari litaingia humu humu ndani utapanda, “ hayo yalikuwa maneno ya askari na maofisa usalama waliomzingira Ponda asitoke nje kwa miguu.

Naye Ponda wakati akitoka nje ya mahakama alisikika akisema: “Sikuachiwa kwa huruma ya mtu, ilikuwa ni haki yangu, kuna kesi nyingine nyingi nzito kubwa ambazo Serikali inashindwa kuzithibitisha.

“Dola inatengeneza kesi nzito hazina ushahidi, inaharibu mfumo wa usalama, kesi zote hizo zinatokana na mashinikizo ya siasa, tuache kutengeneza kesi kwa ajili ya masuala ya siasa.”

Gari aina ya BIGHORN yenye rangi nyeusi ilipoingia ndani ya uzio wa mahakama, Ponda, mkewe na ndugu mmoja waliingia ndani pamoja na maofisa usalama kwa ajili ya kumsindikiza hadi nyumbani kwake.

Ponda alitoka nje ya mahakama akiwa ndani ya gari ambalo lilikuwa likisindikizwa na magari ya polisi wenye silaha.

Waumini wa Kiislamu ambao walikuwa nje ya uzio wa mahakama waliishia kupunga mikono huku wakisema Takbir…Takbir.

Awali akisoma hukumu hiyo, Hakimu Nongwa alisema upande wa mashtaka ulikuwa na mashahidi 16 na upande wa utetezi ulikuwa na mashahidi 53.

Alisema watuhumiwa walikuwa wanakabiliwa na mashitaka matano ambayo ni kula njama, kuingia kwa nguvu uwanja wa Markaz Chang’ombe mali ya Agritanza Limited na kuuzuia kwa nguvu uwanja huo.

Mengine ni kuiba vifaa mbalimbali vya ujenzi vyenye thamani zaidi ya Sh milioni 59 wakati mashitaka ya kushawishi waislamu kukusanyika katika uwanja huo yakimkabili Sheikh Ponda na Salehe Mukadamu.

“Matukio hayo yalitokea kati ya Oktoba 12 na 16 mwaka jana. Shtaka la kula njama halijaeleza washtakiwa walikula njama kutenda kosa gani… mahakama inajiuliza ni kosa gani walikula njama kati ya mashtaka yanayowakabili.

“Katika kesi hii mahakama haijaona hata shahidi mmoja aliyesema jinsi washtakiwa walivyokula njama, mahakama inaona kosa la kula njama halijathibitika, inawaachia huru washtakiwa wote,”alisema Nongwa.

Nongwa alisema shtaka la kushawishi halikusema jinsi Ponda na Mukadamu walivyowashawishi waislamu kukusanyika katika uwanja wa Markaz na hakuna shahidi aliyetaja watuhumiwa walioshawishiwa hivyo shtaka hilo pia halijathibitishwa.

Alisema vilevile hakuna ushahidi kwamba washtakiwa wote ni wafuasi wa Sheikh Ponda.

“Shtaka la pili la kuingia kwa nguvu limethibitika bila kuacha shaka kwamba Sheikh Ponda aliingia katika uwanja huo hivyo anatiwa hatiani. Washtakiwa wengine wote kuanzia wa pili hadi wa 50 katika shtaka hili wanaachiwa huru,”alisema.

Hakimu Nongwa alisema shtaka la kuzuia kwa nguvu uwanja huo halijathibitika kwa sababu hiyo washtakiwa wote wanaachiwa huru katika shtaka hilo na shtaka la wizi pia halijathibitika.

Alisema hakuna ushahidi kwamba msikiti wa muda uliojengwa na akina Sheikh Ponda ulikuwa na thamani ya zaidi ya Sh milioni 59, sawa na thamani ya mali za Kampuni ya Agritanza Limited.

“Naona shaka kama malighafi yote iliyojenga msikiti wa muda ilikuwa mali ya Agritanza Limited, mahakama inatia shaka hivyo kosa la wizi halijathibitika. Washtakiwa wanaachiwa huru kwa shitaka hilo pia.

“Upelelezi katika kesi hii haukufanyika vizuri, ungefanywa vizuri washtakiwa wote wangeweza kutiwa hatiani kwani ukisikiliza ushahidi wao unaweza kuhisi kwamba walishiriki lakini mahakama haiwezi kuwatia hatia kwa vile wenye jukumu la kuthibitisha mashtaka ni Jamhuri,” alisema Nongwa.

Hakimu Nongwa alisema ni jambo lisilobishaniwa kwamba kipande cha ardhi kinachodaiwa kuwa cha Agritanza Limited kina mgogoro.

BAKWATA walibadilishana na Kampuni ya Agritanza Limited bila waislamu wengine kuridhia. Mahakama ya Kisutu haina uwezo wa kumaliza mgogoro wa ardhi hivyo wasioridhika wanatakiwa kufuata taratibu kwa kupeleka madai yao katika Mahakama ya Ardhi.
 
SOURCE: MTANZANIA.
Share this article :

0 comments:

Speak up your mind

Tell us what you're thinking... !

ZILIZOSOMWA SANA.

Followers

Blog Archive

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Proudly powered by Blogger
Copyright © 2011. Kitoloho - All Rights Reserved
Template Design by Creating Website Published by Mas Template