- Kitoloho
Headlines News :
Home » »

Written By Msamaa on Tuesday, May 7, 2013 | 11:22 AM


Jumanne, Mei 07, 2013 06:20 Na Waandishi Wetu, Arusha, Dodoma

*Walikuwa njiani kutoroka kupitia mpaka wa Namanga
*Rais Kikwete akatisha ziara Kuwait, arudi nyumbani

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk. Emmanuel Nchimbi

Mkuu wa Jeshi la Polisi, Said Mwema

JESHI la Polisi mkoani Arusha linawashikilia kwa mahojiano watu wenye asili ya Kiarabu wanaotuhumiwa kulipua kwa bomu Kanisa Katoliki jijini Arusha na kusababisha vifo vya watu watatu na wengine 59 kujeruhiwa.

Akitoa kauli ya Serikali bungeni jana, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk. Emmanuel Nchimbi, alisema kati ya hao, yumo kijana Victor Ambrose (20), ambaye ni dereva wa bodaboda anayetuhumiwa kurusha bomu hilo.

Kuhusu watuhumiwa wengine watano, Dk. Nchimbi, alisema wanne kati ya hao ni raia wa kigeni ambao hakutaja nchi zao na mmoja ni Mtanzania, ambao wanashikiliwa kwa mahojiano.

Kauli ya Serikali, imekuja siku moja baada ya bomu kulipuka wakati wa ibada ya uzinduzi wa parokia mpya ya Mtakatifu Joseph Mfanyakazi, Parokia ya Olasiti, jijini Arusha.

Dk. Nchimbi aliwataja waliofariki dunia katika mlipuko huo ni Regina Longino Kurusei, Mwarusha (45), mkazi wa Olasiti na majeruhi mwingine James Gabriel (16) aliyefariki usiku wa kuamkia jana.

Mlipuko huo, ulitokea baada ya kuanza kwa uzinduzi wa parokia hiyo ambapo mgeni rasmi alikuwa Balozi wa Vatican nchini na mjumbe wa Baba Mtakatifu, Askofu Fransisco Mantecillo Padilla.

“Wakati mgeni rasmi akiwa ametoka nje ya kanisa akijiandaa kukata utepe kama ishara ya uzinduzi, mtu mmoja alirusha kitu chenye ukubwa wa ngumi kuelekea eneo la mkusanyiko wa watu.

“Uchunguzi wa awali, unaonyesha mlipuko huo ni bomu. Uchunguzi wa kubaini aina ya bomu lililotumika unaendelea kufanywa na polisi kwa kushirikiana na askari wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ),” alisema.

Alisema katika siku za hivi karibuni, kumekuwa na watu wanaopandikiza chuki za kidini kwa lengo la kutaka kuleta mapigano na mauaji miongoni mwa Watanzania.

“Sina shaka shambulio la Arusha ni sehemu ya mikakati hiyo ovu, nataka niwahakikishie Watanzania kuwa Serikali haitavumilia hata kidogo mbegu za chuki za kidini miongoni mwa wananchi.

“Tutachukua hatua kali bila huruma kuzikandamiza njama hizi mbaya dhidi ya taifa letu. Tutachukua hatua kali kwa mtu yeyote bila kujali hadhi na nafasi yake katika jamii. Amani yetu kwanza mengine baadaye,” alisema.

Alisema kutokana na tukio hilo, tayari maelekezo yametolewa na kikosi kazi kimeundwa kushirikiana na vyombo vingine vya ulinzi na usalama kuchunguza tukio hilo.

Alisema mwaka 2012, mgombea mmoja wa urais nchini Marekani wakati wa uchaguzi aliishutumu Serikali kutokana na tukio la kulipuliwa ubalozi wa Marekani nchini Libya.

“Ni wazi kuwa mgombea huyu alichukua tatizo lile kama ajenda ya kisiasa. Hata hivyo alishutumiwa vikali na Wamarekani wenzake kwamba ni mtu aliyekosa uzalendo kwa taifa lake.”

BALOZI PADILLA
Naye Balozi wa Papa nchini, Askofu Mkuu Francisco Montecillo Padilla, aliwatembelea na kuwapa pole majeruhi wa mlipuko wa bomu waliolazwa Hospitali ya Mkoa wa Arusha ya Mount Meru na ile ya St. Elizabeth.

Askofu Padilla, alipita wodi za majeruhi na kuwajulia hali majeruhi wote, huku akiwaombe wapone haraka.

Huku ulinzi mkali ukiwa umeimarishwa, Askofu Padilla aliongozana hospitalini hapo na Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Arusha, Joseph Lebulu.

Akitoa tamko kwa vyombo vya habari jana hospitalini hapo, baada ya kuwatembelea majeruhi, Askofu Lebulu, alisema daima wataendelea kusimamia mafundisho ya Yesu Kristo yanayowataka kuushinda ubaya kwa wema.

Alisema Yesu Kristio katika mafundisho yake aliwasihi wafuasi wake kuhakikisha hawalipizi kisasi kwa jambo lolote.

“Yesu Kristo, anatuambia tunatakiwa kuushinda ubaya kwa wema, sisi tunathamini sana maisha ya mtu kuliko kitu kingine chochote, kwani tunatambua mtu ameumbwa na Mungu.

“Wala hatuwezi kumdhulumu mtu kutokana na itikadi yake ya dini yake, kwani Yesu Kristo ametufundisha katika shida tusilipize kisasi.

“Anatutaka tuwe tayari kuushinda ubaya kwa wema, hili tutalizingatia. Sasa anayediriki kuua wenzake tunaamini hana Mungu ndani yake au tuseme ni kazi ya shetani, kwani hiyo ndio kazi yake,” alisema Askofu Lebulu.

Akizungumzia kuhusu ulinzi kuimarishwa katika maeneo mbalimbali, Askofu Lebulu, alisema hata kama ulinzi utaimarishwa bado ni sawa na kazi bure, kwani amani siku zote hailindwi kwa ulinzi.

Alisema ulinzi unaweza kusaidia tu, lakini jambo kubwa tunapaswa kujiuliza ni kwa nini mambo haya yanaendelea kutokea tena bila wasiwasi.

“Amani haiwezi kuimarishwa, kama mioyo ya watu imeoza huwezi kutegemea binadamu azuie uhalifu. Sasa labda katika tukio la juzi tungeweza kusema ni mwizi, lakini ni mwizi gani anayetupa bomu kanisani?” alihoji Askofu Lebulu na kuongeza:

“Huyu alikuwa anatafuta nini kanisani mpaka atupe bomu watu wakiwa wanasali, anatafuta nini, ndani yake kuna uovu mkubwa sana,” alisema.

Askofu Lebulu aliendelea kueleza kwamba ipo haja ya kuondoa mizizi ya ugaidi ulioanza kusambaa nchini kwa kuitaka Serikali iliyopo kusimamia, kutafuta na kueleza wananchi wake huku akiitaka Mahakama itoe uamuzi wa yanayostahili.

Alisema inashangaza kuona maisha ya watu yakiendelea kupotea bila sababu za msingi, kwani hakuna hasara kubwa zaidi waliyopata kama maisha ya watu waliokufa na kujeruhiwa katika eneo la mlipuko huo.

“Nimemuona yule mama pale uwanjani, sitamani hata kuelezea na yule mtoto mdogo jamani watu wale, wameuawa bila hatia yoyote,” alisema.

JK akatisha ziara
Habari zilizotolewa jana na Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu mjini Dar es Salaam, zilisema Rais Kikwete, ameamua kukatiza ziara yake ya kiserikali nchini Kuwait ili kurejea nyumbani kutokana na tukio la shambulio la kigaidi la mlipuko mjini Arusha, ambako watu wawili wamefariki na 60 wamejeruhiwa.

Rais Kikwete, aliyekuwa aondoke kesho kurejea nyumbani, amelazimika kukatiza ziara hiyo na anaondoka Kuwait City kurejea nyumbani mara moja, ili kuwa karibu na wafiwa pamoja na majeruhi.

Miongoni mwa shughuli ambazo hazitafanyika sasa kutokana na uamuzi huo wa Rais, ni ziara ya kutembelea Kampuni ya Mafuta ya Kuwait katika eneo la Ahmadi mjini Kuwait, hatahudhuria dhifa ya chakula cha jioni ambacho alikuwa anaandaliwa na Waziri Mkuu wa Kuwait, Sheikh Jaber Al Mubarak Al Hamad Al Sabah.

MAJERUHI
Kwa upande wake, Kaimu Mganga Mkuu wa Hospitali ya Mkoa, Dk. Mariamu Murtaza, alisema mpaka sasa hospitalini hapo kuna majeruhi 31, huku kati ya hao, watatu wakiwa na hali mbaya.

“Majeruhi watatu hali zao si nzuri, tumelazimika kuwafanyia upasuaji wa tumbo, mapafu. Lakini pia watoto wawili nao hali zao si nzuri. Na mmoja wao, James Gabriel (16) alifariki juzi akiwa safarini kupelekwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, alisema Dk. Mariamu.

Alisema kufariki kwa majeruhi James, sasa kumefanya idadi kufikia watu wawili, baada ya mwanamke aliyejulikana kwa jina la Regina Loning’o, huku idadi ya majeruhi waliolazwa ikiwa ni 66 hadi jana.

“Kwa kweli tunaishukuru Bohari ya Dawa ya Taifa (MSD) kwa kutupatia msaada wa dawa tulizozihitaji kwa wakati, kwani tumeweza kufanya kazi hadi saa 4 usiku kutokana na kupokea wagonjwa wengi kwa wakati,” alisema Dk. Mariam.
Share this article :

1 comment:

  1. Tunalaaani kwa nguvu zote vitendo visivyojali utu na ubinadamu vinavyofanywa na watu ambao kwa sasa ni kujidanganya kusema ni akina nani waliohusika vyenginevyo pawepo na ajenda ya siri dhidi ya kundi tuhumiwa. Ila kimsingi tunapaswa kujenga utamaduni wa kuheshimu afya na damu za watu wengine mana si utu wala uungwana na ni dhambi kubwa kupoteza roho za watu.

    ReplyDelete

ZILIZOSOMWA SANA.

Followers

Blog Archive

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Proudly powered by Blogger
Copyright © 2011. Kitoloho - All Rights Reserved
Template Design by Creating Website Published by Mas Template