- Kitoloho
Headlines News :
Home » »

Written By Msamaa on Sunday, May 19, 2013 | 2:12 PM


MABADILIKO YA KWELI YANATOKANA NA UAMUZI MGUMU.

MUSTAKABALI wa nchi yenye amani na mafanikio ya kiuchumi miongoni mwa jamii; yapo mikononi mwa wananchi wenyewe na sio wanasiasa. Wanasiasa ni wananchi miongoni mwa wananchi ambao hufuata miongozo ya chama cha siasa. Miongozo hiyo inaposhindwa kufikia malengo yaliyokusudiwa kwa hulka na mifumo inayofuata chaguo la mikondo ya kimataifa, huufumbia macho utu kwa kulazimisha wananchi kufikiri vile wanavyotaka wao wafikiri. Kazi kubwa ya chama cha siasa ni kushika hatamu katika nchi. Ukisikiliza hoja za baadhi ya wachambuzi kuhusu mwelekeo wa nchi, mmeng’enyo wa kifikra na matokeo ya chambuzi zao, yanahalalisha matukio kwa hoja nyepesi kwamba; yanayotukia hayawezi kuepukika kwa kuwa hata nchi zilizoendelea zilipitia katika aina ya matukio yanayoipitia nchi yetu.

Kwa chambuzi hizo, wananchi wanaambiwa kutii mabadiliko kwa njia yoyote, iwe ya kufa na kumwaga damu, basi mathalani ni matazamio ya kisiasa wanastahili kupata stahili ya kile wanachotarajia kukipata kupitia siasa za wakati. Hata kama mwananchi atapitiwa na kitu chenye ncha kali tumboni, usoni, mdomoni, kifuani anatakiwa kutii mapito, kwa kuwa kwa kufanya hivyo itamsadia kufikia kule walikofikia wengine katika nchi zilizoendelea. Chambuzi hizi ukizipasua na kuona “utumbo” uliomo ndani yake kama umekaa sawasawa, majibu ya wakati kutokana na vipimo vya wakati utabaini kwamba wale waliokuwa wakitazamiwa kielimu kuwa viongozi wenye fikra mpya, bado wana matatizo ya urithi wa kufikiri.

Matatizo ya urithi wa kufikiri ni janga ambalo pia limejielekeza katika siasa za nchi kupitia mifumo ya urithi wa kimataifa. Hisia na mihemuko ya kisiasa inatatiza mwelekeo sahihi wa nchi. Ni wananchi pekee ndio wenye uwezo wa kuiweka nchi katika hali ya amani na mafanikio kwa njia ya kujitambua pale walipo na wapi wanataka kwenda; na wanatumia njia ipi kufikia matazamio yenye afya endelevu. Viongozi wa siasa waliotoa ahadi mwaka 2010, wameanza kuandaa ulaghai wa mwaka 2015 dhidi ya wananchi wangali bado hawajatekeleza ahadi walizoahidi.

Mbaya zaidi, Bunge letu limepewa majina kama vile bunge la mipasho, bunge la komedi, bunge la kampeni, nani anajali maisha yako? Je, inatosha kusema bunge letu la mipasho? Je, inatosha kushabikia siasa zisizo na shibe kwa wananchi? Je, nini matokeo ya ushabiki wa kisiasa? Kwa ufupi, wanasiasa wanahujumu akili zetu kupitia njia za hatari ilihali wao wakibaki salama na familia zao. NIONAVYO MIMI; wananchi lazima watimize wajibu wao kwa kufanya kazi na kukataa viongozi wenye malengo binafsi. Malengo ya kisiasa yaliyojikita katika kuwagawa Watanzania kwa itikadi za kidini na maeneo ni lazima yazikwe kupitia fikra mpya za wananchi. Lazima wananchi wapaze sauti dhidi ya matumizi mabaya ya kodi zao kwa kuwalipa wabunge wachafuzi wa lugha, badala ya kujadili mambo ya msingi, vinginevyo tungemtumia babu wa kifimbo cheza awachape bakora. Wananchi watambue na kujitambua kwamba wao ndio taa ya nchi.

NIONAVYO MIMI; siasa za nchi zinapoteza mwelekeo na kutoleta tumaini lolote kwa wananchi, hivyo ni wajibu wa wananchi kutambua hilo linahitaji fikra zao mpya badala ya zile za urithi kwamba ni kipindi cha mpito. Haya ni maneno ya wavivu wa kufikiria ambao fikra zao zimeganda na kukosa mwelekeo unaofaa kuzuia hatari itokanayo na mapito. Hisia na mihemko ya uchu wa madaraka ni ajenda ya siasa ambazo bila wananchi kujitambua na kuzidhibiti, siku si nyingi tutashuhudia hali ya hatari ikijitokeza miongoni mwa jamii zisizokuwa na hatia. Lazima wananchi waache upofu walionao wa kufikiri upande mmoja wa kubeba vipofu wenzao wasioona kwamba hawahusiki katika mambo ya maendeleo ya wananchi. Tuache kumung’unya maneno.

 

SOURCE:www.kiongozi.co.tz/
Posted by Mhariri Kiongozi May 2, 2013.
Share this article :

0 comments:

Speak up your mind

Tell us what you're thinking... !

ZILIZOSOMWA SANA.

Followers

Blog Archive

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Proudly powered by Blogger
Copyright © 2011. Kitoloho - All Rights Reserved
Template Design by Creating Website Published by Mas Template