- Kitoloho
Headlines News :
Home » »

Written By Msamaa on Tuesday, May 7, 2013 | 10:34 PM

Ugaidi wa Arusha umewaumbua tena polisi

Bwana Mdogo.
SIKU iliyopangwa kuwa ya kupokea wanajeshi wetu mashujaa waliorejea nchini kutoka Uganda mwaka 1979, sherehe kubwa katika Kata ya Malangali ziliandaliwa katika viwanja vya Shule ya Sekondari Malangali.
Ilikuwa siku ya furaha. Wanajeshi walisimulia walivyomtia adabu nduli Idd Amini Dada, walieleza walivyolisambaratisha Jeshi la Uganda lililokuwa na vifaa vingi na zaidi umakini wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na umahiri wa kitengo cha upelelezi.
Msemaji Mkuu wa wanajeshi wale alijinasibu kuwa Tanzania ni ya tatu duniani baada ya Shirika la Ujasusi la Marekani (CIA) na Mosad ya Israel, kwa uwezo wa kuchunguza mbinu za maadui na kuzivuruga.
Alisema hata uwezo wa kuchunguza matukio maovu yaliyotekelezwa na adui Tanzania ina uwezo mkubwa.
Masimulizi mengine ya kivita hayakuwa yanasikika kutokana na wananchi kushangilia kupita kiasi na kina mama walipiga vigelegele kusifu majeshi yetu.
Hiyo ilikuwa Malangali tu, kwingineko nchini kulikuwa na hadithi za kusisimua, kutia moyo. Ya Dar es Salaam sikuyajua, mimi nilikuwa Malangali.
Leo nikiwa kwenye chumba cha habari najiuliza kimetokea nini hadi maadui wa amani yetu wanaingia nchini, wanapanga nyumba zetu, wanatengeneza vilipuzi na kufika kwenye eneo na kuhujumu bila wanajeshi wetu kujua?
Leo nikiwa ndani ya chumba cha habari, najiuliza kimetokea kitu gani hadi Jeshi la Polisi limebaki kutegemea msaada wa Shirika la Upelelezi la Marekani (FBI) kwa matukio ambayo hata raia wanayajua?
Nachelea kuunga mkono hoja ya wapinzani kwamba Jeshi la Polisi livunjwe, lakini ukweli limekuwa mzigo, limesahau au limeacha majukumu yake, limebaki kuwa kitengo maalumu cha propaganda na mkono wa mateso wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Bila FBI, polisi wetu hawawezi kuchunguza tukio lolote na wakifanya watatoka na matokeo ya ajabu. Walichunguza tukio la kutekwa na kuteswa kwa Dk. Steven Ulimboka wakatoka na mtuhumiwa ambaye Dk. Ulimboka anasema siye.
Mpaka leo wameshindwa kumkamata aliyemtesa Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri, Absalom Kibanda; na mbaya zaidi polisi wameshindwa kuwanasa polisi saba waliomzingira mwandishi wa habari wa Kituo cha Channel 10, Daudi Mwangosi, wakamsulubu na hatimaye kumlipua kwa bomu la machozi.
Uwezo wa polisi wetu umedorora tangu mwanzoni mwa miaka ya 1990. Kipindi hicho polisi hawakubaini njama zilizopangwa na Waislamu wenye msimamo mkali kwenda kuvamia na kuvunja mabucha ya nguruwe katika eneo la Manzese, Dar es Salaam. Mwanazuoni mmoja maarufu wa Kiislamu alitajwa kuhusika.
Aidha, tukio la Agosti 7, 1998 la kulipuliwa kwa Ubalozi wa Marekani nchini liliwaumbua polisi wetu; hawakujua hata pa kuanzia.
Watu 11 walikufa na 85 walijeruhiwa. Polisi wakapata mahali pa kujitetea baada ya muda kama huo siku ileile Ubalozi wa Marekani nchini Kenya kulipuliwa na kusababisha vifo vya watu 212 na majeruhi karibu ya 4,000.
Hapo ndipo tulishuhudia polisi wetu wakihamanika, simu na ‘radio call’ mikononi lakini walikuwa wanazuga tu. Makachero wa FBI walipokuja ndio walibaini magaidi hao kwamba waliingia nchini Juni 1998.
FBI ndio waligundua kwamba waliolipua ni kikundi cha Egyptian Islamic Jihad cha nchini Misri chenye fungamano na al-Qaeda ambacho kilisema kitazungumza na Marekani kwa lugha inayoijua vema.
FBI walibaini kwamba mawakala waliingia nchini wakapanga nyumba moja eneo la Ilala na walikuwa wanatumia gari aina ya Suzuki Samurai. Ukweli makachero walipata taarifa nyingi na gereji iliyotumika katika kuandaa boksi.
Makachero hao walifanikiwa kumnasa Ahmed Ghailani wa Zanzibar na kueleza kuwa ni wakala wa kikundi hicho chenye uhusiano na kikundi cha al-Qaeda kilichokuwa kinaongozwa na Osama bin Laden.
Badala ya kutumia mafunzo waliyopata kwa ajili ya kuihami nchi, polisi wetu wakayatumia mafunzo hayo kupambana na kuvikomoa vyama vya upinzani. Akili zao zikawa kwenye siasa – wapewe ukuu wa wilaya, ukuu wa mkoa na ubunge.
Polisi Zanzibar wakawanasa na kuwabambikia kesi ya uhaini Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad na baadaye Juma Duni Haji na wenzake 18 wakabambikiwa kesi kama hiyo wakafungwa.
Mwaka 2001 polisi waliwapiga wafuasi wa CUF waliokuwa wanaandamana kwa amani eti intelejensia yao ilibaini kwamba walitaka kuteka kituo cha polisi na kuchukua silaha. Wafuasi wapatao 27 walichinjwa kwa risasi.
Kwa vile, serikali ilishapitisha sheria ya ugaidi, mwaka 2005 walijifungia wakachora mchoro wa ugaidi na namna nzuri ya kuwabambikia CUF ili kuinusuru CCM.
Hapo aliibuka aliyekuwa Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Omari Mahita, akatangaza kuwa CUF wameingiza majambia kwa ajili ya kuanzisha machafuko baada ya Uchaguzi Mkuu mwaka ule.
Japokuwa tuhuma zile ni za kigaidi, Mahita aliishia hapo, hakumkamata mtu wala kumshtaki yeyote kuhusiana na madai hayo.
Mahita hakueleza waliyakamata kwenye meli, ndege na idadi na hakueleza viongozi waliohusika na hatua alizochukua. Kwa hofu watu waliipigia tena CCM ikapeta.
Katika matukio makubwa ya ugaidi kama huu wa kulipuliwa Kanisa Katoliki la Parokia ya Mt. Joseph Mfanyakazi, Olasiti, Arusha, intelejensia ya polisi iko mahututi.
Wakati Machi 13, 2013 polisi waliitangazia dunia kumkamata kwa tuhuma za kupanga ugaidi, Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa CHADEMA, Wilfred Lwakatare, makanisa zaidi ya 30 yamelipuliwa nchini, baadhi ya viongozi wa dini kuuawa na wengine kujeruhiwa vibaya, polisi hawajui.
Kinachosikitisha ni kwamba, polisi si tu wameshindwa kubaini njama mapema, kama wanavyofanya kwa wanasiasa, bali pia hawana uwezo hata wa kupeleleza.
Mifano ni kama ifuatavyo. Shambulio hilo lililofanywa na mtu asiyejulikana Jumapili ya Mei 5, 2013, wakati wa uzinduzi wa kanisa hilo la Parokia ya Mt. Joseph Mfanyakazi, Olasiti, Arusha, polisi hawakujua licha ya kwamba baadhi walikuwa eneo la tukio.
Jambo zuri waliohusika kurusha bomu na kupanga njama hizo wamekamatwa kwa msaada wa FBI na Interpol. FBI ndio wamesaidia hata Zanzibar kama itakavyoelezwa hapa chini.
Desemba 9, 2011, Kanisa la Silom, Kianga Mkoa wa Kusini Unguja lilibomolewa na watu wanaosadikiwa ni Waislamu wenye msimamo mkali na Kanisa la Pefa la Mtufaani, Mwera, Wilaya ya Magharibi, Unguja lilichomwa moto.
Oktoba 12, 2012 Waislamu wenye msimamo mkali walivamia na kuchoma moto makanisa matano huko Mbagala Wilaya ya Temeke. Madai yao ni kupinga kitendo cha mtoto mmoja wa Kikristo kukojolea juzuu katika mabishano baina ya mtoto huyo na mwenzake wa Kiislamu.
Novemba 6, 2012 Katibu wa Mufti wa Zanzibar, Sheikh Fadhil Suleiman Soraga, kutokana na msimamo wake juu ya uthabiti wa Muungano wa sasa, alimwagiwa tindikali na mtu asiyejulikana wakati akifanya mazoezi huko karibu na nyumbani kwake Mwanakwerekwe.
Desemba 26, 2012 Padri Ambrose Mkenda wa Parokia ya Mpendae, Zanzibar alipigwa risasi na watu wasiojulikana nje ya nyumba yake jioni wakati akitoka kanisani.
Februari 11, 2013 Mchungaji wa Kanisa la Pentekoste Assemblies of God, Mathayo Kachila aliuawa katika vurugu za kugombea uhalali wa kuchinja kati ya Wakristo na Waislamu huko Geita.
Siku sita baadaye yaani Februari 17, 2013 Padri Evarist Mushi aliuawa kwa risasi alipokuwa akielekea Kanisa la Mt. Theresia, Mtoni Zanzibar.
Matukio haya yote, ukiacha la kuharibiwa makanisa Mbagala, kuuawa kwa Padri Mushi na ugomvi wa Geita, polisi hawajawakamata wahusika katika matukio hayo mengine.
Vilevile, polisi walifanikiwa kuwanasa walioharibu makanisa ya Mbagala baada ya kudai ni wahuni tu si Waislamu wenye msimamo mkali. Lakini aliyemuua Padri Mushi alikamatwa na makachero wa FBI.
Ziko wapi tambo kwamba Tanzania ni ya tatu kwa uwezo wa kuchunguza matukio ya kihaini na kigaidi baada ya CIA na Mosad?
Ziko wapi tambo kwamba Tanzania inashika nafasi ya tatu kupeleleza matukio baada ya FBI? Je, ni kutokana na siasa kuathiri jeshi hilo au kukwepa matukio yenye fungamano na dini? Hapa ndipo lilipo tatizo.
Bila FBI polisi hawawezi kunasa magaidi wa ukweli isipokuwa waliopangwa kwa ushirikiano na CCM. Mfano anayetajwa kuwa ndiye alipanga njama za kumteka na kumpeleka eneo la mateso Dk. Ulimboka ni Ofisa Usalama wa Taifa lakini polisi wamemkamata raia wa Kenya.
Kwa vile, katika kipindi kifupi FBI wametusaidia kuwanasa watu 10 waliohusika na mlipuko wa Arusha, na wametusaidia kumkamata mshukiwa wa mauaji ya Padri Mushi, wananchi tunaomba FBI ichunguze pia kupata ukweli wa watu waliomteka, kumtesa Dk. Ulimboka, waliomtesa Kibanda, waliowaua Mwangosi na Issa Ngumba wa Redio Kwizera.
Ikiwa nchi hii itaingia katika machafuko watu wa kwanza kubeba lawama watakuwa polisi.
Miaka ya 1960 polisi ndio waligundua njama za mapinduzi yaliyowahusisha pia Bibi Titi na wengineo.
Polisi weledi na wazalendo waligundua njama za mapinduzi mwaka 1983 na matukio mengine.
Lakini polisi wa leo licha ya kujengewa uwezo wanaua raia na kunyang’anya mali kama kesi ya Abdallah Zombe na wanatesa kama Dk. Ulimboka na Kibanda.
 
CHANZO: TANZANIA DAIMA.
Share this article :

1 comment:

  1. Ndugu yangu jina lako tu linadhihirisha wazi kwamba wewe ni bwamdogo kiasi kwamba kuna mambo unahitaji kusaidiwa ili uwe uelewa wa kutosha. Kukusaidia tu Waislamu tangu uhuru huu upatikane waliandamwa na mpaka leo wanaendelea kuandamwa na moja katika sababu ya kuandamwa ni kwamba wametupwa nje katika viunga vya uongozi licha ya jitihada kubwa waliyoifanya kupigania uhuru huku Nyerere akiwa kama mualikwa kusindikiza jahazi la watu na shughuli zao. Kwa hiyo shutma hizo ulizonazo sisi hazitushangazi dhidi ya Waislamu kwani ndani ya nchi hii wamehalalishiwa majina yote mabaya na pia ni halali nguvu za dola kuwaangukia kwani nchi inaendeshwa kwa mfumo kristo. Sasa kusikia jambo fulani wamesingiziwa wao au kuitwa Wahuni wanapodi haki zao si jambo geni mana wao wanalelewa na mama wa kambo asiyewapenda hata kidogo "Tanzania" Ila hujui kwanini ripoti hazitolewi hadharani baada ya uchunguzi na kukusaidia tu ni kwamba wale ambao hudhaniwa kwamba ndio waliotenda, baada ya uchunguzi huthibitika si wahusika kwani "NGUVU YA DHANA HUZIMWA NA YAKINI"

    ReplyDelete

ZILIZOSOMWA SANA.

Followers

Blog Archive

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Proudly powered by Blogger
Copyright © 2011. Kitoloho - All Rights Reserved
Template Design by Creating Website Published by Mas Template