- Kitoloho
Headlines News :
Home » »

Written By Msamaa on Thursday, May 2, 2013 | 5:15 AM


 TANU
Jimbo la Tanga, 1956
ILIKUWA ni huko Tanga tu katika historia ya Tanganyika kuwa dhana mpya katika siasa zaidi ya ule ubwana wa Wazungu uliongezwa katika uhusiano baina ya Waafrika na Waarabu. Dhana hii iliongezwa ndani ya mfumo wa siasa za Tanganyika ili kuwakinza Waafrika katika siasa. Hiki kilikuwa kitu ambacho Waafrika walikuwa hawajapambana nacho. Kwa zaidi ya karne moja walikuwa wamezoea ubwana wa Wazungu. Jimbo la Tanga lilibarikiwa na kuwa na Waafrika walioelimika sana. Waafrika hawa walikuwa kutoka kabila la Wabondei. UMCA ilikuwa imehama kutoka Zanzibar kwenda Magila katika Jimbo la Tanga mwaka 1875. Ukristo ulianzishwa na kustawi katika nchi ya Wabondei, na vivyo hivyo nafasi za elimu kwa watoto wa Wabondei. Katika lile wimbi la kuwania nafasi za elimu, watoto wengi wa Kiislamu walibatizwa. Ni jambo la kawaida miongoni mwa Wabondei kukuta majina kama Peter Saidi au John Ramadhani. Huu ni ukumbusho wa damu ya Kiislam katika Wabondei. Wabondei wengi walikwenda Makerere College na siasa za kizalendo zilipoanza baada ya Vita Kuu ya Pili, Wabondei walikuwa wamejaa katika utumishi wa serikali ya kikoloni. Gurudumu la historia ya Tanganyika likizungushwa na baadhi ya Wabondei, maarufu miongoni mwao wakiwa watu kama Martin Kayamba aliyejikomba sana kwa wakoloni, George Magembe mtu ambae huku alikuwa hayuko wala kule hayuko, hujui kama yupo na wazalendo au na wakoloni, Stephen Mhando; mzalendo mwenye msimamo mkali na na mdogo wake Peter.
Wabondei walikuwa ndiyo walimu, makarani, wakalimani mahakamani na maofisa wa ustawi wa jamii katika serikali ya kikoloni. Hili lilikuwa tabaka maalum la Waafrika, waliosomeshwa na wamishonari kuitumikia serikali ya kikoloni na katika kufanya hivyo kulitumikia Kanisa na Ukristo, uhusiano ambao ulikuwa wenye manufaa kwa pande zote mbili zilizokuwa zikishirikiana. Ilikuwa vigumu sana kwa Wabondei kutokana na upendeleo huo wasifikirie kwamba wana uhusiano maalum na Kanisa na serikali ya kikoloni. Hawa Waafrika wasomi kutoka shule za misheni na Makerere walikuwa watiifu kwa taasisi mbili zanye nguvu nchini, yaani serikali ya kikoloni na Kanisa. Kwa ajili hii basi, ilibakia kwa Wadigo Waislam wasiokuwa na elimu kama elimu ilivyokuwa ikiitikadiwa, kuunda TANU na kuongoza harakati za kudai uhuru.
Wamishionari waligundua kuwa Wadigo walikuwa wagumu sana kubatizwa na kuingizwa kwenye Ukristo kwa sababu ya imani yao thabiti katika Uislam. Kwa hiyo Wadigo hadi hii leo wamebakia kuwa kabila la Waislam. Baada ya kuukuta Uislamu umeimarika vyema katika pwani ya Tanga, wamishonari kwa kukataa kuhasimiana na Waislam, walianzisha misheni zao ndani zaidi mbali na pwani sehemu inayojulikana kama Misheni ya Magila. Hapa UMCA ilianzisha shule na hospitali. Wadigo walishikilia imani yao ya Kiislamu na wakabakia nyuma katika elimu kwa sababu ya kukataa kwao Ukristo. Kwa jili hii wakajinyima nafasi za kazi za madaraka katika seriklai ya kikoloni. Huku kuwapanga watu kwa tabaka kulikuwa na athari katika kuanzisha upinzani dhidi ya ukoloni kwa kuwa waliofadhiliwa na Kanisa walishindwa kupinga wakoloni kwa kuwa ukoloni na Ukristo walikuwa wamoja.
African Association huko Tanga ilikosa umoja baina ya wale walioitwa 'wasio na elimu na wasiojua kusoma' na wale wasomi ambao kutoka kwao wote hawa chama cha siasa kingeweza kuundwa. Waafrika wasomi, Wabondei waliunda vikundi vyao peke yao vya wasomi kutokana na juhudi za ofisa mmoja wa kikoloni. Vyama hivi vikijulikana kama Discussion Groups 167 yaani, vikundi vya majadiliano, vilitarajiwa kutojihusisha na kisiasa na vilitiwa nguvu na serikali kuhimiza mijadala na kusoma vitabu. Katika muda wote wa uhai wa vikundi hivyo hawa wasomi wa Makerere walikuwa chini ya usimamizi wa afisa Mzungu.
African Association huko Tanga ilitawaliwa na watu wa mchanganyiko wa damu ya Kiarabu na Kiafrika. Hawa walikuwa watu wenye elimu ndogo. Kundi hili halikuwa na mkabala mzuri na Wabondei wengi wao wakiwa Wakristo wenye elimu. Kundi hili lililokuwa na damu ya Kiarabu lilijiona bora kwa daraja kuliko Waafrika weusi. 168 Kama hivi vikundi viwili muhimu vingeweza kuzikusanya pamoja nguvu tofauti zao, vingeweza kuunda umoja wa siasa wenye uwezo mkubwa sana kama ile kamati ndogo ya siasa ya TAA iliyoundwa huko Dar es Salaam. Muungano huu ungeweza kuongoza harakati za kudai uhuru huko na halikadhalika ungeweza kupata mafanikio makubwa kwa kuwashirikisha wananchi katika kudai haki zao. Lakini kama ilivyokuwa, hizi kambi mbili zilikuwa hasimu; kila upande ukijitenga mbali na umma; wengine walijiona bora kwa sababu ya rangi ya ngozi yao na wengine walijiona bora kwa sababu ya elimu yao.
Gavana Edward Twining alipounda Constitutional Development Committee mwaka 1949, na kukaribisha maoni na mapendekezo kutoka kwa raia, TAA Tanga ilijikuta haina uwezo wa kuandika waraka. Uongozi wa Waarabu katika African Association haukuwa na elimu, maarifa au ujuzi uliotakiwa kutayarisha na kuandika waraka kwa serikali. Wasomi wa Makerere katika vile vikundi vya majadiliano waliinyakua fursa hiyo na kuandika waraka ambao uliwakilishwa kwa Gavana Twining.169 Pamoja na ukweli kuwa waraka ule uliandikwa na Waafrika wenye elimu kubwa kwa wakati ule, kwa hakika waraka ulikuwa na upungufu ukilinganisha na ule ulioandikwa na kamati ndogo ya siasa ya TAA, Dar es Salaam.170
Mwaka mmoja baadae, katika mwaka 1951 ujumbe wa Umoja wa Mataifa ulipozuru Tanganyika, kile kikundi cha majadiliano, ingawa si wawakilishi wa wananchi kikifanya kazi yake nje ya TAA, kiliwasilisha waraka kwa ujumbe huo kikionyesha kuwa wao wanawakilisha maoni ya Waafrika. Hili lilizusha mzozo baina ya wasomi wa Makerere na ule uongozi wa Waarabu katika TAA.171 Haya makundi mawili yalijikuta hayana kusudio au muelekeo wenye maana, kidogo kidogo yalisahaulika. Kule Tanga mara chache watu waliihusisha ofisi ya TAA na siasa. Ofisi ya TAA inakumbukwa na kuhusishwa na mahakama ambako Kadhi, Sheikh Ali bin Hemed alihukumu jamii ya Waislam kwa kutumia sharia.
Lakini Tanga iliibuka mwaka 1955 na kukabiliana na serikali ya kikoloni kupitia juhudi binafsi za kikundi cha wafanyabiashara wadogo wadogo katika soko la Ngamiani. Kikundi hiki kiliongozwa na kijana Peter Mhando, katibu wa zamani wa kile kikundi cha majadiliano cha wasomi wa Kibondei. Akikiongoza kikundi hiki ambacho kilikuwa na Waislam, alikuwa baharia mstaafu, Hamis Heri Ayemba. Hamis Heri alikuwa Mmanyema kutoka kabila la Wakusu wa Belgian Congo. Peter Mhando alikuwa akifanya kazi kama mhandisi katia Noran Industries- wanunuzi wa nazi na watengenezaji sabuni pale Tanga. Hamisi Heri alikuwa na umri wa katikati na katika ujana wake alikuwa baharia na alipata kusafiri chombo kimoja na Abeid Amani Karume, ambae baadae alikuja kuwa rais wa Zanzibar. Baada ya Vita Kuu ya Pili, Hamisi Heri alirudi kwao Tanga ili aanze biashara. Heri alikuwa mtu aliyejikuza na kujielimisha mwenyewe; na alikuwa amesafiri sana. Hamisi Heri alizungumza vizuri sana Kiingereza na Kiarabu. Katika miaka yake ya mwanzo katika biashara, alikuwa dalali. Heri aliwashangaza wateja wake kwa uhodari wake wa lugha mbali mbali, akinadi bei kwa Kihindi au Kiarabu, kutegemea utaifa wa watu waliokuwepo pale mnadani.
Harakati za kudai uhuru zilipoanza Heri alikuwa ametajirika na mmoja wa Waafrika wenye kuheshimiwa sana mjini Tanga. Mhando alipochoshwa na kile kikundi cha majadiliano, alijiunga na Hamisi Heri na kikundi cha Waislam wa pale mjni ambao walikuwa wakijitahidi sana kuunda tawi la TANU. Wakati huo mwanasiasa mwenye uzoefu mkubwa kuliko wote mjini Tanga alikuwa Mwalimu Kihere.172 Lakini siasa za mapambano baina ya ule uongozi wa TAA chini ya Waarabu na kikundi cha majadiliano zilimzuia kutoa mchango wowote wa maana. Mwalimu Kihere alikuwa amehudhuria mikutano kadhaa ya African Association tangu mwaka 1946. Wakati wa uongozi wa Abdulwahid Sykes alikuwa amedumisha uhusiano mkubwa sana baina yake yeye mwenyewe binafsi, Abdulwahid na Dossa Aziz. Hii ilifanya vilevile adumishe mawasiliano ya karibu sana na makao makuu ya TAA. Lakini kwa sababu ya mizozo katika siasa hapo Tanga, ule mkutano mkuu wa kuasisiwa TANU uliofanyika Dar es Salaam mwaka wa 1954 ulipita bila ya Tanga kupeleka mjumbe.
Kile kikundi cha wafanyabiashara wadogo wadogo katika soko la Ngamiani kiliitisha mkutano katika Ukumbi wa Tangamano tarehe 5 Septemba, 1955. Waliohudhuria mkutano huo walikuwa Hamis Heri, Peter Mhando, Mohamed Kajembe,173 Tuwa Abdallah, Dhili Mgunya, Abdallah Rashid Sembe, Victor Mkello,174 Mohamed Sadik, Hassan, Peter Ramadhani Jembe na Ali Mohamed. Peter Ramadhani tayari alikuwa mwanachama wa TANU huko Arusha na alikaribishwa mkutanoni ili waasisi wa TANU wanufaike kutokana na uzoefu wake. Wasomi wa Makerere, uongozi wa TAA chini ya Waarabu na Mwalimu Kihere hawakuwepo kwenye mkutano huu muhimu. Mkutano ulifunguliwa na Hamis Heri saa tisa adhuhuri na ulifungwa saa mbili baadae kwa uamuzi kuwa mkutano mwingine wa kuchagua viongozi wa chama ufanyike tarehe 23 Oktoba. Mkutano uliamua vilevile kuwa juhudi zifanyike kupata waanachama wengi iwezekanavyo. Kiasi kidogo cha fedha kilikusanywa na Harir Omari Siagi alipewa aende makao makuu ya TANU, Dar es Salaam kununua kadi sabini za TANU.
Tarehe 23 Oktoba, wanachama wa mwanzo wa TANU huko Tanga walikutana kuchagua uongozi wao chama. Hamisi Heri alichaguliwa kuwa mwenyekiti na Peter Mhando katibu. Jumla ya watu arobaini na tano walihudhuria mkutano huo na wakapewa kadi za TANU. Mwalimu Kihere alihudhuria mkutano ule lakini hakuchaguliwa katika nafasi yoyote ya uongozi. Kamati ya wanachama iliundwa kutokana na wale wanachama kumi na moja waasisi waliokutana katika ule mkutano wa kwanza mwezi uliopita. Kamati hiyo ilikuwa na wajumbe wafuatao: Abdallah Rashid Sembe, Mohamed Kajembe, Victor Mkello, Dhili Mgunya, Ali Mohamed, Abdallah Mohamed na Mohamed Sadik. Peter Mhando alijitolea nyumba yake kuwa ofisi ya kwanza ya tawi la TANU mjini Tanga. Mara tu baada ya mkutano huu wazee wa Tanga wakiongozwa na Makoko Rashid, mwanachama wa zamani wa TAA walianza kufanya kampeni kwa ajili ya TANU. Chama kilipata msukumo mwingine na kuongezeka nguvu wakati Sadik Ali Patwa Muasia tajiri alipoingia TANU.
Patwa alikuwa Muislam wa madhehebu ya Shia. Patwa alikuwa amehamia Tanganyika kutoka Zanzibar mwaka 1918 baada ya kumalizika kwa Vita Kuu ya Kwanza. Pale Tanga Patwa alianzisha kiwanda cha soda na akatajirika. Wakati huo wa zama za ukoloni wakati Waasia wenzake walikuwa wakiwabagua Waafrika, Patwa alikuwa akikaa na Waafrika wa rika lake akinywa nao kahawa. Halikadhalika watoto wake wakawa wanacheza kandanda na vijana wenzao wa Kiafrika katika vilabu vya Tanga. Hili lilikuwa jambo geni na lisilokuwa la kawaida kutoka kwa familia ya Kiasia wakati wa ukoloni. Patwa alisaidia harakati za kudai uhuru kwa hali na mali, na akaifanyia kampeni TANU miongoni mwa jamii yake mwenyewe ya Kiasia. Wakati wa harakati Nyerere alikuwa akifanyiana maskhara na Patwa akimwambia, 'Mzee Patwa baada ya kupata uhuru nadhani tukuteuwa uwe balozi wetu India.' Lakini Patwa hakuiona Tanganyika huru, alifariki kabla ya uhuru kupatikana.
Baada ya kufungua tawi la TANU mjini Tanga, uongozi wa chama ulimwalika Julius Nyerere, Bibi Titi Mohamed, John Rupia na Mbutta Milando kufanya ziara Tanga. Nyerere alifikia nyumbani kwa Hamisi Heri. Ujumbe huu kutoka makao makuu ya TANU ulipata makaribisho makubwa yaliyoandaliwa na vyama vya lelemama ambavyo kwa kawaida vilikuwa vingi sana katika pwani ya Afrika ya Mashariki kutoka Mombasa nchini Kenya hadi Mikindani, Tanganyika. Kiongozi wa akina mama hawa mjini Tanga aliyesaidia kuieneza TANU alikuwa Bibi Mwanamwema bint Sultan, ndugu wa mbali wa mwenyekiti wa TANU Tanga, Hamisi Heri.
Matokeo ya ziara ya Nyerere Tanga ilikuwa ni kumrudisha Mwalimu Kihere katika siasa. Baada ya kushindwa kupata nafasi yoyote katika chama, Mwalimu Kihere alipoteza shauku ya siasa. Nyerere alipokuja Tanga kuifanyia kampeni TANU ndipo Mwalimu Kihere alikaribishwa kujiunga na chama. Mwalimu Kihere alifahamiana na Nyerere mwaka 1946 walipokutana Dar es Salaam katika mkutano wa mwaka wa African Association. Nyerere alipozuru Tanga Mwalimu Kihere alitaka kufanya dhifa nyumbani kwake kwa heshima yake. Uongozi wa TANU, hususan Hamisi Heri na Mzee Makoko walikataa kumruhusu Nyerere kuhudhuria dhifa hiyo kwa sababu Mwalimu Kihere alikuwa hajaonesha kuiunga mkono TANU. Nyerere akitambua utu uzima wa Mwalimu Kihere, uzoefu na sifa yake ya uongozi katika African Association, alishauri uongozi wa TANU Tanga usiache fursa ile ipite bure. Nyerere alitoa hoja kuwa, ilikuwa muhimu kukubali mwaliko wa Mwalimu Kihere na kutumia fursa hiyo kumuomba arudi kwenye harakati kwa kuwa TANU ingefaidika kutokana na uzoefu wake alioupata katika African Association. Kwa ajili ya nasaa hiyo TANU ilikubali mwaliko wa Mwalimu Kihere na Nyerere alihudhuria dhifa ile nyumbani kwa Mwalimu Kihere pamoja na wanachama wengine.
Source: http://www.islamtanzania.org/an-nuur3/287/index.html.

 
Share this article :

0 comments:

Speak up your mind

Tell us what you're thinking... !

ZILIZOSOMWA SANA.

Followers

Blog Archive

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Proudly powered by Blogger
Copyright © 2011. Kitoloho - All Rights Reserved
Template Design by Creating Website Published by Mas Template