- Kitoloho
Headlines News :
Home » »

Written By Msamaa on Thursday, May 16, 2013 | 9:59 AM

Dk. Slaa afunguka
• Afafanua chimbuko la mkataba kati ya makanisa, serikali
CHANZO:TANZANIA DAIMA{January 14, 2013}
na Mwandishi wetu
KWA mara ya kwanza, Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk. Willibrod Slaa, ameweka bayana chimbuko la mkataba wa makubaliano kati ya serikali na makanisa, huku akiwasihi Watanzania kujiepusha na malumbano yenye hisia za udini.
Dk. Slaa alitoa tahadhari hiyo jana katika ufafanuzi wake aliouandika kwenye mtandao wa kijamii wa Jamii Forum, kuhusu mkataba huo (Memorandum of Understanding - MOU) kati ya Baraza la Kikristo Tanzania, Baraza la Maaskofu Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Alisema kuwa amelazima kutoa ufafanuzi baada ya kuona mkataba huo umewekwa kwenye mtandao wa kijamii, huku watu wengi wakiwa wanauzungumzia kwa kupotosha ukweli wa jambo hilo, na kulihusisha na masuala ya udini.
“Kama mnavyoona, mimi nilikuwa nafahamu historia yote, nafahamu MOU, lakini sikuwa nayo. Mtu huwezi kujua kila kitu, na au kuwa na kila kitu, ‘we need to complement each other’.
“Ninarudia kuwaomba wenzangu, tumetumia muda mrefu sana kujadiliana kwa hisia ya aina mbalimbali. Watanzania hatukuzoea huko nyuma kuulizana dini zetu, wala kabila, wala ukanda. Haya mambo tukiyaendekeza taifa letu litakuwa hatarini,” alisema.
Alisema Watanzania wanapaswa kutambua kuwa, kubomoa ni kazi nyepesi, lakini kujenga tena inachukua muda mrefu, na ni kazi ngumu, na wakati mwingine hata ukifanikiwa huwezi kujenga kama ilivyokuwa.
Akifafanua historia ya jinsi na kwanini MOU hiyo ilizaliwa, Dk. Slaa alisema kuwa huko nyuma serikali ilitaifisha shule nyingi za madhehebu ya dini.
Kwamba utaifishaji huo uliendana pia na ardhi, hasa ikizingatiwa kuwa wakati huo shule zilijengwa kwenye maeneo ya madhehebu ya dini na papo hapo kukiwa na kanisa, nyumba za mapadre na vitu vingine.
Alisema kuwa kwenye miaka ya 1980, madhehebu yakataka warudishiwe ardhi yao, hasa ambayo ina majengo mengine yasiyohusiana na shule hizo.
Dk. Slaa alifafanua kuwa, mchakato wa mjadala ulishika kasi mwaka 1986 Baraza la Maaskofu Katoliki (TEC), lilipopitisha azimio rasmi na kumtaka Katibu Mkuu, awasiliane na serikali kuanzisha mchakato wa kufanya upembuzi na kutenga ardhi ya shule rasmi, kutoka kwenye ardhi inayotumika kwa huduma nyinginezo za madhehebu ya dini.
“Wakati huo mimi (Dk. Slaa), ndiye nilikuwa Katibu Mkuu wa TEC baada ya kupokea rasmi kazi hiyo Desemba1985. Wakati huo madhehebu yaliishakudai yarudishiwe shule zao kwa kuwa zimegeuka kuwa aibu kwa kukosa ukarabati, na ziko kwenye hali mbaya sana,” alisema.
Aliongeza kuwa serikali ilikuwa imekataa ombi hilo kwa lengo la kuwa, shule hizo zinawahudumia Watanzania wote bila ubaguzi, jambo ambalo ndilo lilikuwa lengo kuu la utaifishaji, na sababu ya utaifishaji ilikuwa bado inaendelelea.
Dk. Slaa aliongeza kuwa, mawasiliano yalipoanza na serikali, wakati huo kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu na Wizara ya Elimu, serikali iliomba TEC na madhehebu ya dini kwa ujumla, kama yanaweza kusaidia ukarabati wa shule hizo kwa kuwa ziko kwenye hali mbaya na hali ya uchumi wa nchi haikuwa nzuri.
“Wakati mchakato huo kwa upande wa elimu umeanza, kulikuwa pia na mgogoro kati ya serikali na TEC baada ya serikali kuichukua Hospitali ya Bugando kwa utaratibu huo huo wa kuitaifisha,” alibainisha.
Kwamba hospitali hiyo ilikuwa kwenye awamu ya pili ya ujenzi kwa msaada mkubwa wa Shirika la la Maendeleo la Baraza la Maaskofu Katoliki la Ujerumani (Misereor).
Alisema kuwa Katibu Mkuu wa TEC alipowasiliana na wahisani, walikataa katakata kujihusisha tena na ujenzi au ukarabati wa shule au hospitali, vituo vya afya na zahanati, kwa kuhofia kuwa Serikali ya Tanzania imekuwa ikitaifisha huduma hizo bila majadiliano ya aina yoyote.
Wahisani hao walisema hawawezi kuwekeza fedha za walipakodi wao (Ujerumani), lakini walikuwa tayari kuendelea na huduma mbalimbali za kusaidia dawa na elimu kwa shule ambazo bado ziko chini ya madhehebu ya dini kwa kuwa hawawezi kuwaadhibu wananchi na watoto.
Kwa mujibu wa Dk. Slaa, kwa kuwa shughuli zote za Bugando zilikuwa zinaelekea kusimama, na kulikuwa na mgomo kila siku kwa madaktari, manesi na watumishi, serikali ikaomba wajadiliane upya juu ya mambo makubwa mawili.
Mambo hayo ni utoaji huduma katika sekta za huduma za jamii, na kuwa na chombo cha mawasiliano na majadiliano kati ya Ikulu na madhehebu ya dini.
Lakini kwa kuwa madhehebu ni mengi, wakaomba chombo hicho kiundwe na viongozi wakuu wa madhehebu yaliyokuwa yanajulikana kwa mujibu wa sheria.
Hivyo, Waislamu wakawakilishwa na Bakwata, TEC na CCT (kwa madhehebu zaidi ya 60 yaliyoko chini ya Christian Council of Tanzania), na baada ya mashauriano waliunda chombo hicho.
Alifafanua kuwa kutokana na hali mbaya ya shule, serikali iliomba madhehebu ya dini kusaidia ukarabati kwa zile zilizoonekana zitafungwa kutokana na hali mbaya.
“Nasi kwa upande wetu, kwa nia njema ya kuisaidia serikali, lakini pia kuwahudumia Watanzania, tuliwasiliana na wahisani ambao walikazia msimamo wao kuwa hawako tayari kuingia kwenye shughuli za ujenzi wala ukarabati kwa kukosa msimamo wa wazi na wa kisheria wa Serikali ya Tanzania kuhusiana na utaifishaji wa huduma hizo,” alisema.
Katibu huyo aliongeza kuwa, serikali ilipojulishwa ilichukua hatua ya kuanzisha mchakato mzima wa kupata suluhu ya jambo hilo. Ndipo akapewa jukumu hilo, Anne Makinda, wakati huo akiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu.
“Hatimaye, serikali ilikubali kuwa haitataifisha tena na kwa kuthibitisha hivyo, ikawa tayari kuwekeana mkataba na madhehebu ya dini. Ndipo tukaanzisha mchakato wa majadiliano na wahisani, nao katika umoja wao kati ya dhehebu la kikatoliki Ujerumani na Kilutheri pia la Ujerumani, tukaanzisha mchakato wa namna bora ya kutoa huduma za jamii,” alisema.
Hatimaye, makubaliano yalifikiwa na ndipo kikazaliwa chombo kipya, Tume ya Kikristo ya Huduma za Jamii (CSSC), chenye sekretarieti yake, hivyo huduma ya Christian Medical Board ya TEC na CCT, ikavunjwa na kuwekwa chini ya CSSC.
Dk. Slaa aliongeza kuwa, kwa upande wa serikali aliweka saini Edward Lowassa, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu wakati huo. Kwamba TEC na CCT nazo zikawekeana na wahisani mikataba yao ya ndani ili kupata misaada ya ujenzi, ukarabati na uendelezaji wa huduma zote za jamii.
Share this article :

0 comments:

Speak up your mind

Tell us what you're thinking... !

ZILIZOSOMWA SANA.

Followers

Blog Archive

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Proudly powered by Blogger
Copyright © 2011. Kitoloho - All Rights Reserved
Template Design by Creating Website Published by Mas Template