Hatutaki Muungano wa "Mkataba" kwani uliopo ni wa mahaba? - Kitoloho
Headlines News :
Home » » Hatutaki Muungano wa "Mkataba" kwani uliopo ni wa mahaba?

Hatutaki Muungano wa "Mkataba" kwani uliopo ni wa mahaba?

Written By Msamaa on Saturday, May 25, 2013 | 12:50 PM

Makala
Hoja yangu
Hatutaki muungano wa ‘mkataba’ kwani uliopo ni wa mahaba?
Lula wa Ndali Mwananzela
CHANZO: RAIA MWEMA.
Toleo la 253
8 Aug 2012
WAMEIBUKA  watu wanadai Muungano wa “kimkataba”. Miongoni mwa hawa ni pamoja na mwanasiasa mkongwe wa Zanzibar mzee Hassan Nassor Moyo ambaye amewahi kuwa Waziri Bara na Visiwani.
Pamoja naye wamekuwapo viongozi wa kidini na wengine wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar ambao nao – kama watu waliosahau – wanapigia panda “uhuru wa Zanzibar” na kuwa wanataka Muungano wa “kimkataba”. Bado hawajataka kile ambacho sisi watu wa Bara tuko tayari kuwapa – Zanzibar nje ya Muungano. Hatuutaki Muungano wa “kimkataba”!
Sasa, ukiangalia hoja za hawa wanaotaka Muungano wa Kimkataba utaona kuwa zinavutia watu wasiotaka kufikiri tu au ambao wanafikiri kwa kutumia vionjo kuliko chembe za ubongo ambazo Mwenyezi Mungu amewajalia.

Situkani hapa wala sibezi, naelezea ukweli ambao mtu yeyote ambaye anaweza kutumia ubongo wake anaweza kuufikia bila kuhangaika sana. Wanaosema wanataka Muungano wa kimkataba wanataka tuamini kuwa Muungano uliopo sasa ni wa kimahaba (a romantic union).
Sasa mambo ya mahaba kwa kweli hayahitaji makubaliano yenye nguvu ya mkataba. Mambo ya mahaba yanahitaji watu kukubaliana kihisia tu kuwa pamoja na kufurahia maisha yao pamoja bila kuwekeana makubaliano ya aina yoyote.

Muungano wa kimahaba kimsingi ndio unawafanya watu wawe pamoja mwanzoni  na wakiamua kuupeleka mbele uhusiano wao huingia katika mahusiano ya kimkataba yaani ndoa.
Wanaodai kuwa wanataka Muungano wa kimkataba maana yake ni kuwa hawatambui Muungano uliopo ambao ni wa mkataba. Hawa wana sababu kubwa tatu ambazo wanazitumia kuhalalisha mtazamao wao: kwamba, Baraza la Wawakilishi halikuridhia wala kutunga sheria ya kutambua Muungano isipokuwa Bunge la Muungano tu; Abeid Karume aliingia makubaliano ya Muungano akiburuzwa na Julius Nyerere huku Mwanasheria wake Mkuu akiwa hana taarifa na kuwa makubaliano ya awali yalivunjwa baada ya kuongeza mambo kwenye orodha ya Mambo ya Muungano.

Nina uwezo na ningeweza kuzijibu zote hizo zote tatu ili kuonyesha kuwa zina makosa makubwa. Lakini kwa vile si lengo langu kuutetea Muungano pendekezo langu nikuwa Wazanzibari wanaotaka “Muungano wa Kimkataba” wamepotea. Sisi watu wa Bara (najua sizungumzii wote wa Bara!) hatutaki Muungano nje ya huu wa mkataba ili tuingie mkataba mwingine ambao hauwezi kuwaridhisha Wazanzibari hawa.
Tutaweza vipi kuwa na mkataba mpya wa Muungano ambao hautaweka orodha ya Mambo ya Muungano – kwani ukiweka tu mambo ya Muungano tutajikuta pale pale tena.
Tutaweza vipi kuingia makubaliano ambayo yatafanya Zanzibar iwe sawa kwa kila hali na Tanganyika bila Tanganyika kujikuta inabebeshwa mzigo mkubwa? Najua wanaopenda “mkataba” huu mpya watataka Tanganyika na Zanzibar zigawane nusu kwa nusu nafasi mbalimbali (za utawala, ubalozi) na hata mapato mbalimbali.

Lakini nina uhakika pia watu hawa hawatopenda kuchangia nusu kwa nusu kuendesha serikali hiyo ya Muungano. Nitapenda tuwe na mkataba mwingine pale ambapo Wazanzibari wanaotaka kugawana “nusu kwa nusu” wawe tayari kuendesha serikali ya Muungano nusu kwa nusu!
Lakini zaidi ni kutambua vile vile kuwa Muungano uliopo tayari ni wa kimkataba njia pekee ya kutoka hapa ni ama kufanya marekebisho makubaliano hayo au kuyavunja. Binafsi napendekeza kuwa wakati umefika kwa Wazanzibari kuyavunja wao wenyewe kabla sisi watu wa Bara hatujawasaidia kuyavunja makubaliano haya.
Haiwezekani watake “Zanzibar huru” na wakati huo huo kutaka “Muungano wa kimkataba”. Haiingii akilini kwa sababu kama Zanzibar itakuwa “huru” na “full sovereignty” itaweza vipi tena kuingia kwenye mkataba?

Je, kuingia kwenye mkataba mwingine wanafikiria itawezekana bila kusalimisha hakimiya hiyo (without surrendering some sovereignty)? Yaani wawe huru halafu wajiunge bado na nchi nyingine? Si tutarudi hapa hapa tulipo sasa? Yaani, pale ambapo Zanzibar iko huru sana na wakati huo huo bado imeungana.
Wanaotaka Muungano wa Kimkataba wanaitaka Zanzibar na bado wanataka Muungano. Hawawezi kuwa na vyote viwili. Sasa kama nilivyosema huko nyuma sisi watu wa Bara tutawasaidia kutoka kabisa kwenye Muungano kwani tayari tumeshawahi kuwa na muungano wa kimkataba na kamwe wenzetu wameshindwa kuridhika. Tanganyika imekubali kufa ili Zanzibar ipate uhai lakini katika uhai wake Zanzibar inaibeza Tanganyika. Wanatuambia “ifufueni Tanganyika”.
Na bahati mbaya wapo watu wa Tanganyika wanaofikiria Zanzibar ikiondoka itarudi Tanganyika; haiwezekani. Nchi yoyote itakayopatikana baada ya Zanzibar kuondoka haiwezi kuwa Tanganyika!
Kwa vile hadi hivi sasa hakuna Mzanzibari hata mmoja – kati ya wale wanaotaka kuvunjwa Muungano – aliyeleta hoja Bungeni ya mswada wa sheria ya kura ya maoni inaonekana labda tuwasaidie.

Tumesubiri kwa muda wa wiki kadhaa kuona kama kuna Mzanzibar mpinga Muungano ambaye ameweza kuthubutu kuleta mswada wa aina hiyo kwenye Baraza la Wawakilishi au hata kwenye Bunge la Muungano ili Wazanzibari wapige kura ya kuamua kuhusu Muungano. Hakuna aliyejitokeza. Na kushangaza zaidi pamoja na yote wanayosema kuhusu kutaka Zanzibar hakuna Mzanzibari aliyeanza kampeni ya kutaka Wazanzibari walioko kwenye taasisi na idara za Muungano kuachia nafasi zao kususia Muungano ili warudi kujenga Zanzibar yao “mpya”; hakuna ambaye amejitokeza kutaka Wazanzibari walioko Bara wawaunge mkono katika kuukataa Muungano. 
Ndiyo maana tumeanza hii kampeni ya Let Zanzibar Go. Tuiache Zanzibar iende. Na sisi watu wa bara na wale wengine ambao wanaamini bora Zanzibar ijitoe inabidi tuwasaidie kujitoa (kwani hawana ujasiri wa kuamua kujitoa kiukweli).

Njia pekee ya kufanya hivi ni kwa wananchi wa Bara wanapotoa maoni juu ya “muundo wa Muungano” wasikubali kutaka “serikali tatu”. Kwa sababu serikali tatu ndio MUUNGANO WA KIMKATABA huo.
Watu wa Bara wadai serikali moja, taifa moja! Kama serikali mbili za sasa hazifai na haziwekani kwa hakika serikali tatu itakuwa ni mzigo mkubwa. Njia iliyobakia ni kudai serikali moja na taifa moja.
Kwa sababu kama Muungano wa sasa ambao ni wa mkataba hautakiwi tena, bali Muungano mwingine wa kimkataba basi hakuhitajiki kuwapo kwa Muungano mwingine wowote.

Share this article :

0 comments:

Speak up your mind

Tell us what you're thinking... !

ZILIZOSOMWA SANA.

Followers

Blog Archive

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Proudly powered by Blogger
Copyright © 2011. Kitoloho - All Rights Reserved
Template Design by Creating Website Published by Mas Template