- Kitoloho
Headlines News :
Home » »

Written By Msamaa on Tuesday, May 7, 2013 | 10:39 PM

Hatari ninayoiona ni hii...

Maggid Mjengwa
NDUGU zangu, haya ni moja ya maandiko yangu muhimu katika kazi yangu ya uandishi na uelimishaji jamii.
Ni kwa kutambua ukweli kuwa nchi yetu imepatwa na shambulizi la kigaidi.
Imetokea Arusha, ingeweza kutokea popote pale katika ardhi ya nchi yetu.
Tunawapa pole wahanga wa tukio hili. Ni msiba wetu sote. Tuwe sasa na mioyo ya ustahamilivu. Tusikimbilie kunyosheana vidole. Tuwaache tuliowapa dhamana ya kuchunguza waifanye kazi yao. Wajibu wetu wa kizalendo ni kutoa ushirikiano.
Naam, kama nchi, tunapitia sasa kwenye kipindi cha majaribu makubwa. Huu ni wakati wa kuizunguka bendera yetu ya taifa. Ni wakati wa kuonesha umoja, uzalendo na mshikamano wetu kama taifa. Umoja, uzalendo na mshikamano wetu ni silaha muhimu na kubwa kabisa Watanzania tumeendelea kuimiliki tangu enzi na enzi. Ndiyo silaha tunayoendelea kuimiliki hadi sasa.
Tuna lazima ya kupambana hadi risasi ya mwisho kuhakikisha adui hatupokonyi silaha hii.
Ndugu zangu, hii ni nchi yetu. Ni nchi yetu sote, Watanzania wa imani zote. Tutambue sasa kuwa kwenye safari tunayokwenda kama taifa, mbele yetu kuna mawimbi makubwa. Kwa pamoja tutavuka, kwa kugawanyika tutazama.
Wahenga wetu walisema; kamba hukatikia pabovu. Watanzania wa imani tofauti tuna historia ya kuchanganyika na kuishi kwa amani na upendo. Hatuna hulka ya kubaguana. Tukianza sasa dhambi ya kubaguana, basi, itaendelea kututafuna.
Na siku zote, uzoefu ni mwalimu mzuri. Mathalani, uzoefu unatufundisha kuwa kuwasha moto ni jambo jepesi sana, lakini, kuuzima moto ni kazi ngumu sana.
Ona, moto ulioanza kwenye nyumba moja ya nyasi kijijini, waweza kusambaa haraka na hata kuteketeza kijiji kizima. Na tangu utotoni tumetahadharishwa hatari ya kucheza na moto.
Naam, binadamu usicheze na moto, labda iwe kwenye mazingaombwe.
Na ningependa hapa tuyakumbuke maneno ya busara na hekima nyingi kutoka kwa Bi. Joy Mukanyange.
Huyu alikuwa Balozi wa zamani wa Rwanda nchini Tanzania. Mama huyu aliyatamka maneno haya miaka 13 iliyopita, takriban miezi sita kabla ya kifo cha Baba wa Taifa. Bi. Joy Mukanyange alikiona kile ambacho Watanzania hatukukiona.
Ni kama vile alikuwa mtabiri, maana, alichokisema mama yule leo ndiyo tunaanza kukiona. Siku ile ya Aprili 6, 1999, katika iliyokuwa Kilimanjaro Hotel, Bi. Joy Mukanyanga aliyatamka haya:
“Naogopa, kwani nimeanza kuona dalili zinazojengeka za mgawanyiko wa kidini nchini Tanzania na eneo lote la Maziwa Makuu, hali ambayo inaweza kusababisha mauaji ya halaiki kama yale yaliyotokea nchini mwetu mwaka 1994.”
Alisema balozi yule wa Rwanda kabla ya kuendelea kutoa ufafanuzi wa historia ya Rwanda na matukio yaliyosababisha mauaji yale ya Wanyarwanda ya wao kwa wao. Ndiyo, Bi Joy Mukanyange alikiona kile ambacho Watanzania hatukukiona.
Na tutafanya makosa makubwa, kama hata sasa, tutajifanya kuwa hatukioni kile ambacho Balozi Joy Mukanyange alikiona. Watanzania tukubali sasa kuwa tumepatwa na bahati mbaya sana ya baadhi ya Watanzania wenzetu kuanza kupandikiza mbegu za chuki miongoni mwetu. Kuna wanaotaka tuanze kubaguana kwa misingi ya kidini.
Hili ni jambo la hatari sana. Ni hulka ya mwanadamu, anapokuwa matatizoni kumtafuta kondoo wa kafara. Mtu mwingine wa kumnyooshea kidole kwa matatizo yake.
Hali duni ya uchumi wa nchi, hali duni za maisha na umaskini wa watu wetu isiwe chachu ya kuanzisha vurugu za kijamii.
Maana, taratibu tumeanza kuizoea misamiati ya sisi na wao. Mathalani, sisi Wakristo na wao Waislamu. Sisi Wachaga na wao Wazaramo. Tunasahau kuwa katika nchi yetu hii hakuna sisi na wao, kuna sisi tu. Tutakapokumbwa na maafa ya kitaifa watakaoathirika ni sisi, hakutakuwapo na wao.
Hatari kubwa ninayoiona ni tatizo la wengi wetu kuwa na ufahamu mdogo juu ya dunia tunayoishi sasa, kibaya zaidi, ufahamu mdogo wa historia yetu. Hivyo basi, kusababisha hali ya kutojitambua kama taifa.
Ndiyo uelewa wa historia ya jamii husika ni jambo muhimu sana. Kiumbe huwezi kuelewa ya leo, kesho na kesho kutwa kama huelewi ya jana. Kuielewa historia yako ni kuelewa ulipo na unakokwenda. Historia ni kama maji ya mto, yakipita hayarudi. Historia ni wakati, ni muda. Kihistoria jana ni sawa na zamani.
Karne nyingi zilizopita wahenga wetu walitafsiri muda kama mkusanyiko wa matukio ya zamani na sasa. Waliamini kuwa yaliyotokea zamani na yanayotokea sasa ndiyo yenye kusaidia kubashiri yatakayotokea kesho, yataamua mustakabali wetu.
Dalili tunazoziona sasa za kupandikiza mbegu za chuki kwa misingi ya udini si dalili njema. Haya yatatusababishia maafa.
Tuliopata bahati ya kutumia kalamu zetu hatuna budi kuliweka hili hadharani. Ni wajibu wetu wa kizalendo.
Narudia, hii ni nchi yetu. Katika ulimwengu tunamoishi kuna mamilioni ya watu ambao hawana nchi.
Wahenga wetu walishiriki katika kuijenga nchi hii, wametutarajia sisi tuendelee kuijenga na kuilinda heshima na hadhi ya nchi yetu.
Mengine yanayofanyika sasa si tu yanaitia doa nchi yetu, bali, yanaiaibisha nchi yetu.
Ndugu zangu, hatuna haja ya kubaguana kwa misingi ya dini, ukabila na rangi. Sisi wote ni Watanzania. Tuna historia ya kujivunia.
Ni historia yetu wenyewe. Kinyume cha baadhi yetu wanavyofikiri au wanavyotutaka tufikiri, historia yetu haikuanzia enzi za Mwarabu, Mjerumani au Mwingereza. Historia yetu haikuanzia enzi za TANU wala Afro Shiraz.
Na dini hizi za kimapokeo zinazotufanya sasa tufarakane zimekuja na kuzikuta dini zetu za asili, na bado tunazo. Na hakika, Afrika hatugombanii matambiko.
Afrika kila ukoo una tambiko lake, hivyo basi, dini yake. Kamwe hutasikia Waafrika wanagombania matambiko. Hutasikia Waafrika wakigombana kwa tofauti za matambiko yao.
Na sisi ni Waafrika. Hii leo mahala ambapo unaweza kuwagawa Watanzania na hata kufanikiwa kuwafanya wachinjane ni kwenye tofauti zao za imani hizi za kimapokeo; Uislamu na Ukristo.
Naam; kamba hukatikia pabovu. Tusikubali dini iwe ndiyo penye ubovu kwenye kamba inayotuunganisha Watanzania.


0754 678 252.
TANZANIA DAIMA.
Share this article :

0 comments:

Speak up your mind

Tell us what you're thinking... !

ZILIZOSOMWA SANA.

Followers

Blog Archive

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Proudly powered by Blogger
Copyright © 2011. Kitoloho - All Rights Reserved
Template Design by Creating Website Published by Mas Template